Habari

Watuhumiwa kutengeneza mitihani feki ya kidato cha nne

Mwalimu wa shule ya sekondari Hasanga, iliyopo wilayani Mbozi, mkoani Songwe na wafanyabiashara wawili, wanahojiwa na vyombo vya usalama mkoani Mbeya kwa tuhuma za kuhusika na utengenezaji wa mitihani feki ya kidato cha nne.

dsc_0783

Watuhumiwa hao, James Kapinga (36) ambaye anadaiwa kufanya kazi katika Shule ya Sekondari ya Hasanga pia anajitolea kufundisha Shule ya Sekondari ya Wazazi ya Sangu, Baraka Mwazambe (28), mfanyabiashara na mkazi wa Tunduma na mtaalamu wa masuala ya Tehama (IT), Alex Mochi.

Watu hao inadaiwa walikamatwa juzi usiku baada ya mwanafunzi mmoja ambaye jina lake na la shule vimehifadhiwa kukutwa na mtihani wa somo la Kiingereza na alipobanwa, inadaiwa aliwataja wahusika hao.

“Mwanafunzi huyu ni wa shule nyingine tena si ya Mbeya, alikutwa na mtihani feki wa somo la Kiingereza, alipohojiwa alieleza mtihani huo ulitoka Mbeya na Serikali ilipofuatilia iliwabaini wahusika ambao walikuwa wanasambaza mitihani feki,” kilisema chanzo kimoja cha habari hii.

Akizungumzia tukio hilo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Mariamu Mtunguja, alikiri ofisi yake kupokea taarifa juu ya uvujaji wa mitihani na walipofuatilia walibaini mitihani hiyo ni feki.

“Mbeya hakuna mitihani iliyovuja kama inavyoelezwa katika mitandao, ukweli ni kwamba suala hilo lilifuatiliwa ilibainika mitihani inayosambazwa si ile iliyochapishwa na Baraza la Mitihani la Taifa, ni feki na baadhi ya wahusika wanahojiwa na vyombo vya dola,” alisema Mtunguja.

BY: EMMY MWAIPOPO

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents