Habari

Wawili kizimbani kwa tuhuma za kubaka

Wakazi wawili wa Kata ya Sokoni I, Mjini Arusha, wamepandishwa kizimbani kwa tuhuma za kumbaka binti mmoja mwenye umri wa miaka 18 (jina linahifadhiwa).

Mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Arumeru, Devotha Msofe, Wakili wa Serikali, Charles Kagirwa, aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Hilary Juma (20) na Maxmilian Paul (20). Wakili Kagirwa alidai kuwa watuhumiwa hao kwa pamoja walitenda kosa hilo Desemba 22 mwaka jana, katika eneo la Longdong, Kata ya Sokoni I, ambapo walifanya mapenzi na binti huyo bila ridhaa yake.

Alidai kuwa watuhumiwa hao walitenda kosa hilo kinyume cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai, kifungu cha 130 (1),(2),(c) na kifungu cha 137 (1), sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002. Washtakiwa hao walikana kutenda kosa hilo na wakili huyo kuieleza mahakama hiyo kuwa upelelezi wa shauri hilo haujakamilika.

“Upelelezi wa shauri hili bado haujakamilika, tunaomba tarehe nyingine ya kutajwa na suala la dhamana liko wazi kwa washtakiwa kwa masharti yatakayotolewa na mahakama,” alieleza Wakili Kagirwa.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Januari 17, mwaka huu itakapoendelea tena.

BY: Emmy Mwaipopo

chanzo: Mtanzania

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents