Waziri Majaliwa atoa neno kwa watendaji wa serikali
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka watendaji wa Serikali katika ngazi zote wawajibike ipasavyo kwenye ukusanyaji wa mapato na kuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha na rasilimali za Taifa.
Waziri Mkuu amesema Serikali itaimarisha ukaguzi katika ngazi zote na ufuatiliaji wa karibu wa miradi ya maendeleo na kufanya tathmini za mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba miradi na kazi zitakazofanyika zinawiana na thamani ya fedha (Value for money) za umma zinazotolewa na Serikali.
Waziri Mkuu alitoa agizo hilo katika hotuba yake aliyoitoa bungeni wakati wa kuahirisha Mkutano wa 11 wa Bunge jijini Dodoma.
Aidha Waziri Mkuu amesema taasisi zote za Serikali zinasisitizwa kutumia mifumo ya kieletroniki kukusanya mapato na wafanyabiashara wote wanahimizwa kutumia mashine za EFD na kulipa kodi kwa hiari.