Waziri Mkuu aagiza fedha zilizotengwa kujenga ofisi, zijenge hospitali
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameuagiza uongozi wa Halmashauri ya Mji wa Tunduma wilayani Momba kuwa milioni 900 zilizotengwa kwaajili ya kujenga ofisi zianze kujenga ujenzi wa hospitali.
Waziri Majaliwa ametoa agizo jana jioni wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa Shule ya Msingi Tunduma.
Amesema Shilingi milioni 900 zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Halmashauri kwa sasa zianze kutumika katika kuanzisha ujenzi wa hospitali hiyo.
“Kwa kuwa afya ni jambo muhimu katika utekelezaji wa kauli mbiu ya Rais Dkt. John Magufuli ya Hapa Kazi Tu, hivyo naagiza fedha zilizotengwa kuanza ujenzi wa ofisi zitumike katika ujenzi wa hospitali,”alisema Waziri Mkuu.
Hata hivyo, Waziri Mkuu aliuagiza uongozi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) iandae ramani kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo na kuhusu suala la ujenzi wa ofisi Serikali italishughulikia.
Na Emmy Mwaipopo