Habari

Waziri Mkuu apiga marufuku chuo kikuu cha ardhi kukodi makampuni

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amekipiga marufuku Chuo Kikuu Ardhi kukodi makampuni ya kufanya kazi mbalimbali kwa niaba yake.

Amesema kitendo hicho kinaharibu kazi na sifa ya chuo hicho kwa kuwa baadhi ya makampuni wanayoyapa kazi hayakidhi vigezo.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo, kwenye ufunguzi wa sherehe za maadhimisho ya miaka 10 ya Chuo Kikuu Ardhi.

“Kama kuna umuhimu wa kufanya kazi na kampuni ni bora muanzishe kampuni ya kwenu itakayofanya kazi vizuri ili kujiepusha na matatizo.”

Pia Waziri Mkuu amekiagiza chuo hicho kufanya tafiti zenye kuleta majibu ya maswali na changamoto mbalimbali zinazolikabili Taifa na Dunia.

Ametaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni mabadiliko ya tabia nchi, ujenzi holela, uharibifu wa mazingira na majanga ya asili kama mafuriko.

Amesema Serikali inaamini kuwa matokeo ya kazi zinazofanywa na chuo hicho zikiwemo tafiti ni chachu ya maendeleo ya taasisi za elimu ya juu.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Dira ya Maendeleo ya Taifa imeweka mkazo wa kuifanya Tanzania kuwa na uchumi wa kupato cha kati ifikapo 2025, hivyo wanahitajika wataalamu wa kutosha na wenye weledi.

“Hivyo Chuo Kikuu cha Ardhi kama taasisi ya Serikali inawajibu mkubwa wa kutayarisha wataalamu mbalimbali wa sekta za ujenzi, ukadiriaji majenzi na uhandisi wa mazingira.

Pia Waziri Mkuu amewataka watumie fursa hiyo ya kuadhimisha miaka 10 ya chuo hicho kujitafakari na kuona ni kwa namna gani wanaweza kuwekeza zaidi ili kuongeza tija ya uwepo wa taasisi hiyo kwa jamii na Taifa kwa ujumla.

“Wekeni mikakati madhibuti itakayowezesha chuo kupiga hatua kubwa zaidi katika kipindi cha miaka 10 ijayo. Siku zote mjikite katika kutafuta kuwa na ubora zaidi ya wakati uliopita.”

Awali, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako alisema Serikali inakkitegemea chuo hicho katika kufanikisha ajenda yake ya uchumi wa viwanda kwa kuwa kinatoa wataalamu wengi.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na Mkuu wa chuo hicho ambaye ni Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa David Msuya, Mwenyekiti wa Baraza la chuo Bibi Tabitha Siwale, Makamu Mkuu wa chuo Profesa Evaristo Liwa pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali, wanafunzi na watumishi wa chuo hicho.

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

ALHAMISI, NOVEMBA 23, 2017.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents