Habari

Waziri wa Iran atoa onyo kali kwa yoyote atakayeshambulia nchi hiyo atasababisha vita kamili

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Iran amesema shambulio lolote dhidi ya nchi yake, kufuatia hujuma dhidi ya miundombinu ya mafuta ya Saudi Arabia litasababisha vita kamili na kuongeza mvutano katika Guba ya uajemi.

Iran | Mohammad Javad Zarif (citna)

Tamko hilo la waziri wa mambo ya kigeni wa Iran Mohammed Javad Zarif, limewakilisha onyo kali la Iran katika kipindi kirefu cha kiangazi, kilichogubikwa na mashambulio na matukio kadhaa ya kukanganya kufuatia kuporomoka kwa makubaliano yake ya nyuklia na mataifa yalio na nguvu duniani baada ya rais Donald Trump kuiondoa Marekani katika makubaliano hayo.

Tamko lake hilo pia linaangaliwa kama jibu kwa Waziri wa Mambo ya kigeni wa Marekani Mike Pompeo ambaye siku moja iliyopita alipokuwa akielekea Saudi Arabia aliyataja mashambulio hayo kama “tukio la vita.”

Alipoulizwa na shirika la habari la CNN ipi athari ya shambulio la Marekani na Saudi Arabia kwa taifa lake, Zarif alisema anatoa taarifa muhimu kwamba Iran isingelipenda kuingia katika majibizano ya kijeshi lakini pia akasema hawatofumba macho kulilinda taifa la Jamhuri ya Iran.

Ameongeza kuwa vikwazo vyoyvote vilivyowekwa na Marekani kwa taifa lake baada ya kujiondoa katika makubaliano ya nyuklia, inabidi viondolewe kabla ya kufanyika majadiliano ya aina yoyote, huku akisema Marekani imefanya kila iwezalo lakini bado haijaifikisha Iran kuinyenyekea kwa kuipigia goti.

Pompeo asema Marekani inapendelea suluhisho la amani kwa mzozo uliopo

USA Außenminister Pompeo reist nach Saudi-Arabien (picture-alliance/dpa/J. Martin)

Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Mike Pompeo

Kwa mujibu wa shirika la habari la Deutsche Welle, Wakati huo huo Waziri Mike Pombeo ambaye tayari ameshawasili katika Umoja wa Falme za Kiarabu, amesema Marekani inapendelea suluhisho la amani kwa mzozo huo.

Awali alikutana na mwanamfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman mjini Jiddah kujadili shambulio la vituo vyake muhimu vya mafuta, lililosababisha kupungua nusu ya uzalishaji wa bidhaa hiyo muhimu.

Waasi wa Houthi wa nchini Yemn wanaoungwa mkono na Iran walikiri kuhusika na shambulio hilo la Saudi Arabia lakini Marekani inasisitiza kuwa Iran ndio waliotekeleza shambulio hilo.

Urusi kwa upande wake kupitia waziri wake wa mambo ya kigeni Sergei Lavrov imeyataka mataifa yote katika Guba ya uajemi kukaa chini kwa mazungumzo ya kuondoa mvutano uliopo.

Vyanzo: ap/afp/Reuters

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents