Habari

Bodi ya EWURA yakagua bomba la mafuta TAZAMA

 

Mwenyekiti wa Bodi ya EWURA, Prof. Mark Mwandosya ameongoza wajumbe wa Bodi hiyo na Menejimenti kwenye ziara ya ukaguzi katika Bomba la Mafuta la TAZAMA linaloanzia Dar es Salaam, Tanzania hadi Ndola, Zambia. Ziara hiyo ilianza Machi 21, 2025.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati ya Bodi, Ngosi Mwihava alisema lengo la ziara hiyo ni kukagua uendeshaji wa bomba la TAZAMA na masuala yote ya kiuchumi na kimiundombinu

“Moja ya jukumu la EWURA katika sekta ya petroli ni kudhibiti miundombinu inayohusu ya usafirishaji wa mafuta na gesi asilia, hivyo ziara hii ni mahususi kwa ajili ya kukagua bomba, kuona changamoto zilizopo na kuangalia namna tunavyoweza kusaidia utatuzi wa changamoto hizo ili kuendelea kuboresha huduma za usafirishaji wa mafuta kupitia bomba hili” alisema.

Mwihava aliongeza pia kuwa ziara hiyo ni fursa ya Bodi ya EWURA na ya Udhibiti wa Nishati Zambia (ERB) kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali ikiwemo ya upangaji wa bei, mikakati ya uhifadhi wa mafuta ya akiba na kujengea wataalamu uwezo

Ujumbe huo umetembelea kituo cha Chilolwa cha kuangalia usalama wa bomba la mafuta, kituo cha kusukuma mafuta kilichopo Chinsali na ghala la kuhifadhia mafuta lililopo Mpika.

Maeneo mengine yaliyotembelewa ni kituo cha Kilonje cha kusukuma mafuta, kituo cha Mulilima cha kutuma na kupokelea kifaa cha kufanya usafi wa bomba, na kituo cha kupokelea mafuta cha Bwana Mkubwa terminal ambacho kiko Ndola.

Ujumbe huo pia utakutana na uongozi la Bomba la TAZAMA, Bodi ya Wakurugenzi ya Taasisi ya Udhibiti wa Nishati Zambia (ERB) pamoja na Baraza la Mazingira Zambia (NWASCO) ili kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kisekta.

Written by Janeth Jovin

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents