Habari

Bunge la Uganda lapitisha mswada wa kuwafunga jela wapenzi wa jinsia moja

Bunge la nchini Uganda limepitisha mswada wa sheria inayoharamisha kujitambulisha kama mpenzi wa jinsia moja, huku wale wanaokutwa na hatia hiyo wakikabiliwa na kifungo cha hadi miaka kumi jela.

Shirika la kutetea haki la Human Rights Watch linasema kwamba – ikiwa sheria hiyo itaidhinishwa na Rais Yoweri Museveni – sheria hiyo mpya itakuwa ya kwanza mahali popote duniani kuharamisha watu kujitambulisha kama wapenzi wa jinsia moja, watu waliobadili jinsia au watu wanaofanya mapenzi kinyume na maumbile yao.

Uganda ni mojawapo ya nchi zaidi ya thelathini za Afrika ambazo tayari zimepiga marufuku mapenzi ya jinsia moja.

Wabunge wa upinzani walilitaka bunge kutoidhinisha mswada huo, lakini spika wa bunge Anita Among amesema maadili na utamaduni wa nchi hiyo lazima ulindwe.

Chini ya sheria iliyopendekezwa, marafiki, familia na wanajamii watakuwa na wajibu wa kuripoti watu walio katika mahusiano ya jinsia moja kwa mamlaka.

Vitendo vya wapenzi wa jinsia moja tayari ni haramu katika nchi hiyo ya Afrika mashariki.

Lakini mswada huo unalenga kwenda mbali zaidi na kuwafanya watu kuwa wahalifu kwa msingi wa utambulisho wao wa kijinsia.

Mswada huo ambao uliwasilishwa kwa mara ya kwanza mapema mwezi huu, ulipitishwa kwa uungwaji mkono mkubwa katika bunge la Uganda siku ya Jumanne.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents