Diamond ashauriana na BASATA maboresho ya tuzo za muziki Tanzania
Kupitia ukurasa wa Instagram wa @basata.tanzania wameandika kuwa:-
“Msanii wa Bongo Flava nchini Tanzania,na Mkurugenzi wa WCB, Diamond Platnumz akiongozana Mhe.Hamis Shaban a.k a Babu Tale ambaye ni Meneja wa WCB na Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki(CCM) leo tarehe 2 Julai 2023 ametembelea ofisi za Katibu Mtendaji-BASATA Dkt. Kedmom Mapana kujadiliana masuala mbalimbali yanayoweza kusaidia katika Maendeleo ya Sanaa nchini.
Majadiliano hayo yamejikita zaidi kwenye uboreshaji wa Tuzo za Muziki ili ziweze kuvutia wadau wengi kutoka maeneo mbalimbali Duniani.
Aidha, mwanamuziki huyo Diamond ametumia nafasi hiyo kuushukuru uongozi na Menejimenti yote ya BASATA kwa namna wanavyoshadidia wasanii kuwa wawezeshaji zaidi Jambo linaloimarisha Uhusiano baina ya wasanii na Serikali yao.
Diamond pia amesisitiza kuwa yeye pamoja na washirika wake ataendelea kuburudisha na kuielimisha jamii kupitia kazi zake akizingatia Maadili ,mila na desturi za Kitanzania.
Aidha aliwashauri Wasanii wenzake kuwa wawekezaji katika Sanaa hususan Muziki badala ya kufanya Muziki kwa mazoea lakini pia amempongeza Katibu Mtendaji wa BASATA Kedmon Mapana Katika mradi mkubwa wa kutafuta Mdundo wa Taifa kitu ambacho amesema ni jambo muhimu sana kwa hivi sasa hasa kwa wanamuziki wa Kitanzania.
Amemalizia kwa kuliomba Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kuandaa programu maalum ya kutoa elimu kwa Wasanii na wawekezaji kuhusu suala la mikataba kwani itasaidia kuepusha migogoro ya mara kwa mara inayotokea kati ya Wasanii na wawekezaji.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa BASATA, Dkt. Kedmon Mapana amemhakikishia Msanii Diamond Platnumz kuwa Baraza la Sanaa la Taifa BASATA lipo tayari kushirikiana na Wasanii pamoja na Wadau wote katika kuleta maendeleo ya sekta ya Sanaa nchini kwani BASATA ipo katika kuwawezesha Wasanii na Wadau wa Sanaa.
@wizara_sanaatz @pindi.chana @saidiyakubu1 @kmapana @diamondplatnumz