Didier Drogba apata ‘degree’ ya heshima Ivory Coast
Didier Drogba amekabidhiwa ‘degree’ ya heshima kutoka Chuo Kikuu Ivory Coast kutokana na mchango wake katika mchezo wa mpira wa miguu nchini kwao pamoja na kusaidia kurudisha hali ya utulivu katika taifa hilo la Afrika Magharibi.
Mchezaji huyo wa zamani wa Klabu ya Chelsea amesifiwa kwa mchango wake wa kurejesha amani Ivory Coast. Drogba amesaidia mwaka 2005 kupigania nafasi ya kufuzu michuano ya kombe la Dunia.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 43, aliwahi kuwaalika waandishi wa habari katika chumba cha kubadilishia nguo wachezaji ‘dressing room’ baada ya kumalizika kwa mchezo wao dhidi ya Sudan na kuzungumzia machafuko ya miaka mitano ya wenyewe kwa wenyewe katika taifa hilo la Afrika Magharibi.
Drogba pia amekuwa akijihusisha na misaada mbalimbali katika kipindi chake chote alipokuwa akicheza mchezo wa soka, kuna wakati aliwahi kutoa paundi milioni tatu (Mil 3) kutoka kwenye sehemu ya mkataba wake na Pepsi ambapo alizitumia kwa kujenga Hospitali nchini Ivory Coast.