Elimu yaigawa Dunia- Antonio Guterres
Katika kikao maalumu wa kilele kuhusu elimu kabla viongozi wa dunia kukutana kwa mkutano wa hadhara kuu ya Umoja wa Mataifa, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema kila mtu anafahamu elimu huyabadili maisha, uchumi na jamii mbalimbali lakini tunafahamu pia kwamba lazima tuifanyie mageuzi kwa sababu elimu iko katika mgogoro mkubwa. Amedokeza kuwa kiasi asilimia 70 ya wanafunzi wenye umri wa miaka kumi katika nchi masikini hawawezi kusoma. Ima hawaendi shule au wako shule lakini hawasomi vizuri.
“Elimu inageuka kwa kasi kuwa nyenzo kubwa inayosababisha mgawanyiko. Mifumo ya elimu haizingatii sana kwamba elimu haina mwisho na walimu hawajapokea mafunzo wakahitimu vizuri, hawathaminiwi na wanalipwa mishahara midogo. Na pengo la ufadhili wa elimu linaendelea kutanuka kuliko ilivyowahi kushuhudiwa.”
Guterres ameutahadhirisha mkutano kwamba janga la ugonjwa wa Covid-19 lilisababisha athari kubwa kwa elimu, huku wanafunzi maskini wakikosa teknolojia na mizozo ikitatiza masomo shuleni. Amezitolea wito nchi zote zitoe kipaumbele kuongeza matumizi ya fedha kwa kila mwanafunzi huku kukiwa na maswali mengi kuhusu uchumi wa dunia.
Elimu ya wasichana iimarishwe
Katika ripoti iliyochapishwa mapema mwezi huu shirika la maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP lilisema ugonjwa wa Covid-19 ulirudisha nyuma maendeleo ya binadamu kwa miaka mitano. Guterres pia aliutaka utawala wa Taliban nchini Afghanistan ufute vikwazo vyote kuhusu elimu kwa wasichana na iwaruhusu waendelee na masomo katika shule za sekondari.