Habari

Gairo yaja na mikakati ya ufaulu wa Elimu

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma Mwassa amesema Mkoa wa Morogoro umejipanga kuhakikisha kwamba unainua Ufaulu huku akisisitiza umuhimu wa Shule zote kutoa chakula cha mchana, kudhibiti Utoro na Kuwapa walimu mafunzo ya Kuwajengea Uwezo pamoja na kuimarisha Ulinzi na Usalama wa watoto dhidi ya vitendo vya ukatili ikiwemo ulawiti.

Mhe. Mwassa ameyasema hayo katika Kilele Cha Wiki ya Elimu na Tuzo za Kiongozi wa Elimu Gairo iliyoandaliwa na Wilaya hiyo ikiwa ni Mkakati Maalumu wa Kuinua kiwango Cha Ufaulu wa Wanafunzi wa Shule za Msingi na Sekondari.

“Kipekee nimpongeze Mkuu wa Wilaya kwa juhudi hizi za kipekee za kuhakikisha tunajikwamua kutoka hapa kwenda nafasi nyingine. Suala la Mtoto kufaulu kama alivyosema Mkuu wa Wilaya lina pande nyingi. Kuna upande wa Jamii kwa maana wazazi, Kuna upande wa Walimu, watoto na Serikali. Ili mambo yawe mazuri lazima kila upande utimize wajibu wake. Mimi nina hakika kwa mipango hii mwakani mtafika asilimia 80%” alisema Bi Mwassa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Gairo Mhe. Jabiri Makame alisema, baada ya Wilaya kushuka katika ufaulu, Uongozi wa Wilaya kwa kushirikiana na walimu walikaa pamoja kubaini changamoto na kuja na programu ya Kukuza Ufaulu ambayo ilihusisha ziara ya hamasa ya Elimu kwa wazazi, viongozi wa Vitongoji, Vijiji na Kata Katika kudhibiti Utoro, upatikanaji wa chakula shuleni, kufuatilia Maendeleo ya Wanafunzi na kuimarisha Ulinzi na Usalama wa watoto wakiwa shuleni na nje ya Shule, sambamba na uelimishaji wa Jamii kuhusu uanzishaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Elimu Wilaya ya Gairo.

Aidha, walimu wapatao 900 walipatiwa mafunzo ya siku tatu ya Kuwajengea Uwezo wa kutumia Mbinu za Ufundishaji na Ujifunzaji, Mafunzo ya Uongozi kwa Wakuu wa Shule, Walimu Wakuu na Maafisa Elimu Kata, Mafunzo ya Ulinzi na Usalama wa Mtoto na masuala ya Elimu ya Afya ya Akili.

Katika hatua nyingine Kilele Cha Wiki ya Elimu kilihitimishwa kwa kutoa Tuzo za Kiongozi wa Elimu ambazo zilihusisha motisha ya fedha taslimu, Vyeti na Ngao kwa makundi ya Walimu waliofanya vizuri katika masomo yao, Wanafunzi wenye Ufaulu nzuri, Shule Zilizofanya Vizuri katika Taaluma, Viongozi wakiwemo Wakuu wa Shule, Walimu Wakuu na Maafisa Elimu Kata walioonesha Uongozi katika kutekeleza Majukumu yao.

Naye Mwenyekiti wa CCM Gairo ndugu Dastan Mwendi na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Gairo Mhe. Rachel Nyangasi walisisitiza umuhimu wa kutoa chakula Cha mchana Shuleni ili kukuza Uelewa wa watoto shuleni.

Wilaya ya Gairo Mwaka huu imeshuhudia kushuka kwa kiwango Cha Ufaulu katika mitihani ya Shule za Msingi na Sekondari ambapo kwa Mwaka 2022 Wilaya ilifaulisha kwa wastani wa 53% kwa darasa la saba na 85% katika Kidato cha nne.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents