
Jeshi la magereza nchini Afrika Kusini limesema litapinga uamuzi wa mahakama uliomrudisha rais wa zamani Jacob Zuma jela.
“Baada ya kuchunguza hukumu hiyo kwa makini, Huduma za Marekebisho ina uhakika kwamba mahakama nyingine inaweza kufikia uamuzi tofauti,” Idara ya Huduma za marekebisho(DCS) ilisema katika taarifa.
Mahakama ya Juu ya Rufaa Jumatatu iliamuru Bw Zuma arejee gerezani baada ya kushikilia uamuzi wa awali kwamba msamaha wake wa matibabu ulikuwa kinyume cha sheria.
Zuma mwenye umri wa miaka 80 alihukumiwa kifungo cha miezi 15 mwaka jana kwa kudharau mahakama kutokana na kukataa kutoa ushahidi wake wakati wa uchunguzi wa ufisadi.
Lakini aliachiliwa baada ya miezi miwili jela, baada ya mawakili wake kudai kuwa alikuwa na ugonjwa usiojulikana na alihitaji matibabu ambayo hayangeweza kutolewa gerezani.