Michezo

Jezi ya SportPesa Simba,haitafutika kirahisi…

Safaris yao pamoja itaendelea kubaki kwa miaka mingi sana

MWAKA 2017, ndio klabu ya Simba iliingia mkataba wa miaka mitano na kampuni kubwa ya masuala ya michezo ya kubahatisha ya SportPesa Tanzania.

 

Mkataba wa udhamini ambao unaifanya Simba na watani wao Yanga kuingia kwenye rekodi mpya ya klabu zenye udhamini mkubwa zaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki kwa kuwa zinapokea kitita cha hadi Sh bilioni 1.3 kwa mwaka mmoja, haijawahi kutokea katika soka nchini.

SportPesa imeandika rekodi ya kuwa kampuni inayotoa udhamini mkubwa zaidi nchini katika michezo na Simba ni timu ambayo imeutumia vizuri zaidi udhamini huo kujikomboa kuliko watani wao wa jadi, Yanga.

 

Simba sasa ni tishio, si Tanzania pekee, bali Afrika Mashariki na kati na gumzo Afrika lakini hakuna ubishi kwamba wadhamini wao wakubwa na waliosaidia mabadiliko makubwa wakiwa chachu ni SportPesa.

Ligi Kuu Tanzania Bara

Wakati SportPesa wanaingia mkataba wa kuidhamini Simba mwaka 2017, Simba ilikuwa haijagusa ubingwa wa Tanzania Bara kwa misimu minne mfululizo.

Katika misimu hiyo minne, watani wao wa jadi Yanga walikuwa wameubeba ubingwa huo kwa mara tatu mfululizo na Azam FC mara moja.

 

Achana na hivyo, kuna wakati hata kushika nafasi ya tatu ilikuwa shida. Kama unakumbuka msimu wa 2013/14, mabingwa walikuwa ni Azam FC, wakafuatiwa na Yanga halafu Mbeya City na Simba wakitupwa nje ya tatu bora ya Ligi Kuu Bara.

Msimu uliofuata wa 2014/15, Simba ikarejea katika kiwango cha nafuu na kufanikiwa kushika nafasi ya tatu huku Yanga wakiwavua ubinwga Azam FC ambao walirudi katika nafasi ya pili.

Safari ya mapambano ikahamia 2015/16, Yanga wakaendeleza ubabe, Azam FC wakabaki nafasi ya pili na Simba wakaendelea kubaki katika nafasi ya tatu.

Msimu wa 2016/17, Simba wakajitutumua na kupanda hadi katika nafasi ya pili huku Kagera Sugar wakiiondoa Azam FC katika nafasi ya tatu. Hata hivyo, Simba haikuweza kuivua Yanga ubingwa baada ya kulingana pointi lakini mabao ya kufunga na kufunga yakawa ni mzozo.

Huu ndio msimu wa nne wa Simba kabla ya Sportpesa kuingia nao mkataba mwaka 2017, wakati ambao safari ya mabadiliko ya maisha mapya ya kikosi hicho yalianza.

Rafiki yangu mmoja mdau wa mpira aliwahi kuniambia anachukizwa na viongozi wa Simba wanavyoichukulia SportPesa poa. Kwamba hawaijali au kuitimizia mambo kadhaa, sikuwa na uhakika kama hilo linatokea. Lakini nikamuambia kama wanafanya hivyo, basi watakuwa wasahaulifu au wanajisahaulisha.

Sijawahi kuwasikia SportPesa wakilalamika kuhusiana na Simba kutotimiza yaliyo katika mkataba lakini kama ni hivyo, hata wao wanatakiwa kukumbuka kwa kuwa safari waliyosafiri na SportPesa imekuwa na mafanikio makubwa na hawapaswi kuwasarau hata kidogo.

Umeona misimu minne waliyokosa ubingwa na mara moja hata katika tatu bora wakiwa nje. Lakini misimu minne ya SportPesa, mfululizo mara tatu wamechukua ubingwa na dalili zote kuwa msimu wanne ambao ni huu, wanaweza kuwa mabingwa tena.

Safari ilianza 2017/18 na Simba wakabeba ubingwa wakiwa na pointi 69 mwishoni mwa msimu, nafasi ya pili ikaenda Azam FC wakiwa na pointi 58 na watani wao Yanga wao baada ya kubeba ubingwa mara tatu mfululizo, wakavuliwa na kutulia katika nafasi ya tatu wakiwa na pointi 52.

Msimu uliofuata ukiwa wa pili wakiwa na SportPesa, yaani 2018/19, Simba wakabeba tena ubingwa, msimu huu wakiwa moto zaidi baada ya kukusanya pointi 93, Yanga wakapanda hadi nafasi ya pili wakiwa na 86 na Azam FC wakashuka hadi namba tatu wakiwa na pointi 75.

Simba hawakupunguza kasi, msimu wa 2019/20, wakachukua ubingwa kwa mara ya tatu mfululizo na kuwajibu watani wao Yanga. Safari hii wakiwa na pointi 88, Yanga wakafuatia wakiwa na 72 na Azam FC pointi 70 wakiwa katika nafasi ya tatu.

Sasa ni msimu huu wakiwa wanaonekana pia wana nafasi ya kuwa mabingwa tena na wapinzani wao wakiwa watani wao Yanga.

Katika misimu hii minne, Simba wameandika rekodi ya kipekee. Wamecheza Ligi ya Mabingwa na kufanikiwa kufika hatua ya robo fainali mara mbili, kumbuka mara ya mwisho kuingia hatua ya robo fainali ilikuwa ni mwaka 2003.

Bila ya ubishi, Simba bora zaidi ni hii ambayo imepatikana katika kipindi wadhamini wakuu wakiwa ni SportPesa, hakuna ambaye anaweza kuwatoa katika historia ya hili lililotokea.


Simba ya msimu wa 2020/21, ndiyo bora zaidi kwa maana ya kiwango. Kwa wale ambao walikuwa wakipinga, hakuna anayesema tena, hakuna anayeinua mdomo na kusema inapendelewa, hakuna anayejaribu kusema inabahatisha badala yake kila mmoja asiyependa mwendo wa Simba anachofanya labda iwe dua mbaya kimyakimya.

SportPesa wapo katika historia na rekodi hii, inawezekana wako wanaotaka kupinga lakini viongozi na mashabiki wa Simba wanalijua hilo.

Viongozi wa Simba wanastahili pongezi kubwa, maana unaweza kusema vipi Yanga, kwani nao wanapewa udhamini kama huo wa SportPesa lakini vipi. Kweli, viongozi wa Simba wamekuwa bora zaidi na walichofanya pamoja na ubora wa mambo mengine, wameutumia vizuri sana udhamini wa SportPesa pamoja na nyongeza kutoka Azam TV na Mo Xtra kuunganisha nguvu na kufanya mambo yaende kwa uhakika zaidi.

Si vibaya kusema Simba hii ya kipindi cha SportPesa, imekuwa Simba hasa na yenye mafanikio makubwa na tayari historia ya Simba na kampuni hiyo kubwa ya michezo ya kubahatisha hakuna anayeweza kuifunta.

SportPesa imebadilisha kadhaa katika mpira wa Tanzania kama ambavyo unaona iliweza kuzidhamini timu kadhaa na Namungo FC imekuwa moja ya timu zilizoandika rekodi ya kuingia hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho.

Hatua hiyo si ndogo, ni kubwa tena sana na hasa kwa timu kama Namungo FC ambayo hata katika Ligi Kuu Bara ni wageni. Unaona, ndani yake kuna mchango wa Sportpesa kama sehemu ya wadhamini na hii inakufanya uone kweli, mchango wa kampuni hiyo ni mkubwa sana na umesaidia kuleta mabadiliko makubwa katika mpira wa Tanzania.

Achana na kwamba walizidhamini timu kama Singida United na zikawa tishio, lakini historia ya kampuni hiyo na udhamini wake Simba, itaendelea kuzungumza kwa miaka mingi sana ijayo na jezi yenye SportPesa kifuani, itapita katika miaka mingi ya historia ya Simba na soka la Tanzania, kama kumbukumbu yenye mifano isiyoisha.

Kubet mechi za Simba, Yanga na Namungo FC bonyeza hapa

Habari zaidi kuhusu SportPesa.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents