Habari

Mhe Tundu Lissu kufanyiwa upasuaji mwingine, Awaomba jambo Watanzania

Licha ya afya ya Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki, Mhe Tundu Lissu kuimarika, Lissu amesema kuwa mwezi huu atafanyiwa upasuaji mwingine kwenye mguu wake wa kulia.

Mhe. Lissu mwenye magongo akiwa kwenye mazoezi Ubelgiji

Mhe Lissu amesema kuwa upasuaji huo utafanyika tarehe 14 Machi, 2018 katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven, Gasthuisberg ambako amekuwa akitibiwa tangu mwezi Januari.

Wapendwa wangu, Naomba niwape taarifa ya maendeleo yangu ya kiafya. Ninaendelea vizuri na matibabu. Mguu wa kulia unaendelea kupata nguvu na sasa ninaweza kusimama kwa miguu yote bila msaada wa magongo. Hata hivyo, timu ya madaktari bingwa wa mifupa wanaonitibu, wamenitaarifu kwamba kasi ya mfupa wa juu ya goti kuunga ni ndogo sana. .

“Madaktari wangu wamesema kwamba wasipoingilia kati na kurekebisha mfupa huo, kwanza, itachukua muda mrefu sana kuunga; na pili, hata ukiunga baada ya huo muda mrefu, hautaunga kwa namna itakayoondoa hatari ya kuvunjika siku za mbeleni. Kwa sababu hizi, madaktari wangu wamependekeza kufanya operesheni nyingine kwenye mfupa wa juu ya goti la kulia. Hivyo, siku ya Jumatano ijayo ya tarehe 14 March, 2018, nitarudi Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven, Gasthuisberg, kwa ajili ya kufanyiwa operesheni hiyo,“ameeleza Mhe Tundu Lissu kwenye taarifa yake.

Kwa upande mwingine Lissu amewahakikishia Watanzania kuwa yupo kwenye mikono salama na kuwaomba msaada wa hali na mali.

Niko kwenye mikono salama ya kitabibu. Madaktari wangu, Prof. Dr. Stefa Nijs na Prof. Dr. Willem-Jan Mertsemakers, ni madaktari bingwa wa mifupa wanaosifika barani Ulaya kwa utaalamu wao katika fani hiyo. Hivyo, msiwe na hofu. Mungu wetu aliyeniwezesha kuwa hai sasa, ataendelea kutenda miujiza yake kupitia kwa madaktari bingwa hawa. Nitaendelea kuwataarifu maendeleo ya matibabu yangu kadri itakavyokuwa lazima na muhimu kufanya hivyo. Kama kawaida, nawaombeni muendelee kutuunga mkono mimi na familia yangu kwa maombi na misaada ya kibinadamu ya hali na mali kwa kadri ya Mungu alivyowajalia. “ameeleza Mhe. Tundu Lissu.

Mhe Lissu yupo nchini Ubelgiji kwa matibabu baada ya tukio la kushambulia kwa risasi mwaka jana mjini Dodoma na watu wasiojulikana.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents