Habari

Mke wa El Chapo Emma Coronel Aispuro alivyokamatwa Marekani kwa Ulanguzi wa mihadarati (+ Video)

Mke wa mlanguzi mkuu wa mihadarati kutoka Mexico El Chapo Guzman amekamatwa nchini Marekani kwa tuhuma za ulanguzi wa mihadarati , imesema mamlaka nchini humo.

Emma Coronel Aispuro , mwenye umri wa miaka 31 alikamatwa katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Dulles nje ya mji mkuu wa Washington DC.

Anashtakiwa kwa kushiriki katika njama ya kutaka kusambaza dawa aina ya Cocaine, Methamphetamine, heroin na bangi.

Guzman kwasasa anahudumia kifungo cha maisha jela mjini New York kwa kuhusika katika ulanguzi wa mihadarati na fedha.

Jamaa huyo mwenye umri wa miaka 63 ni kiongozi wa zamani wa kundi la walanguzi wa mihadarati wa Sinaloa ambalo ndilo lililokuwa na mtandao mkubwa wa usambazaji wa mihadatari nchini Marekani.

 

Kesi yake mwaka 2019 iligundua mambo ya kushangaza kuhusu maisha yake , kutoka kuwapatia wasichana mihadarati na kuwabaka wakati alipokuwa na umri mdogo wa miaka 13 mbali na kuwaua baadhi ya wanachama wa genge hilo na wapinzani.

Bi Coronel Aispuro anatarajiwa kuwasilishwa mbele ya mahakama ya kijimbo mjini DC kupitia kanda ya video , imesema idara ya haki nchini humo.

Mbali na kukabiliwa na mashtaka ya ulanguzi wa mihadarati , pia anatuhumiwa kushirikiana na wengine kumsaidia mume wake kutoroka jela nchini Mexico 2015.

Alitoroshwa katika jela ya Altiplano nchini Mexico baada ya wanawe kununua jumba lililokuwa karibu na jela hiyo na kuingiza aina ya saa ya GPS ndani ambayo iliwaonesha wachimbaji jela ambayo el Chapo alikuwa anazuiliwa.

Alitoroka kwa kutumia pikipiki ndogo ndani ya handaki hilo.

Stakhabadhi za mahakama zilisema kwamba bi Coronel Aispuro alidaiwa kuhusika katika kupanga kumtorosha mume wake katika jela nyengine kabla ya kufurushwa nchini Marekani mwezi Januari 2017.

Hajatoa tamko lolote kuhusu mashtaka yanayomkabili. Bi Coronel Aispuro ana uraia wa mataifa mawili Marekani na Mexico na amezaa pacha na Guzman.

Alihudhuria kesi ya mume wake iliochukua miezi mitatu mjini New York kila siku , ambapo alisikia kuhusu mashtaka ya mauaji na ubakaji mbali na madai kwamba mume wake alikuwa akimpeleleza yeye na wanawake wake wengine.

Alisalia mtiifu , akisema mwisho wa kesi hiyo kwamba : Simjui mume wangu jinsi mahakama inavyojaribu kumuonesha , lakini nampenda kwa kuwa mwanadamu ambaye nilikutana naye na kuoana naye.

Guzman alitoka katika familia masikini katika jimbo la Sinaloa , kaskazini magharibi mwa Mexico.

Biashara yake ya uhalifu uliopangwa ilikua kubwa na kumfanya kuorodheshwa katika jarida la Forbes miongoni mwa watu matajiri duniani 2009 katika nafasi ya 701 akiwa na mali yenye thamani ya $1bn.

Bofya hapa chini kutazama.

https://www.instagram.com/tv/CLoCNEVBeLA/

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents