Shirika la Afya Duniani WHO, limeonya kwamba robo ya watu ulimwenguni kote ikiwa ni watu bilioni 2.5, wanatabiriwa kuwa watapoteza kiwango fulani cha uwezo wa kusikia ifikapo mwaka 2050.
Kwenye ripoti yake ya kwanza ya ulimwengu kuhusu hali ya kusikia iliyotolewa leo, shirika la WHO limesema ikiwa hatua haitachukuliwa, basi watu wasiopungua milioni 700 katika idadi hiyo, watahitaji huduma za kusikia au masikio kufanyiwa marekebisho.
Ripoti hiyo inaainisha juhudi za kuzuia na kushughulikia tatizo la kupoteza uwezo wa kusikia. Mkuu wa Shirika hilo Daktari Tedros Adhanom Ghebreyesus amesema kutotibu tatizo la kupoteza uwezo wa kusikia, kunaweza kusababisha athari mbaya katika mawasiliano baina ya watu.
Shirika la WHO limekadiria kwamba watu bilioni 1.1 walio na umri wa kati ya miaka 12 hadi 35 wako katika hatari ya kupoteza uwezo wa kusikia kwa sababu ya kelele katika mazingira.