Papa Francis ahimiza amani Congo na Sudan Kusini
Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis amewahimiza watu na viongozi wa nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Sudan Kusini kufungua ukurasa mpya na kupisha njia za upatanisho, amani na maendeleo.
Francis ameyasema hayo katika ujumbe kwa njia ya video jana Jumamosi, ikiwa ni siku ambayo alipanga kuanza ziara ya wiki nzima ya kuhiji katika nchi hizo mbili.
Kiongozi huyo alisitisha ziara yake mwezi uliopita kutokana na maumivu ya goti. Katika ujumbe wake, Papa Francis amewataka watu wa nchi hizo kutokosa matumaini licha ya vurugu, machafuko ya kisiasa, unyonyaji na umaskini ambao amesema umewaumiza kwa muda mrefu.
Aidha kiongozi huyo amewahimiza viongozi wa kisiasa kuwa wana deni kubwa la kutimiza malengo ya vijana ambao ndoto yao ni amani.