Habari

Wajasiriamali na Wakulima Wadogo wapigwa msasa Jijini Tanga

Benki ya NBC imeahidi kuendelea kutoa huduma zake kwa kuzingatia mikakati na mahitaji ya wateja wake wakiwemo wajasiriamali na wakulima kwa kuendelea kutoa mafunzo ya biashara na kilimo biashara kwa wakulima ili waweze kukuza mitaji yao sambamba na kuendesha shughuli zao kwa ushindani.

Meneja Maendeleo ya Biashara Benki ya NBC tawi la Tanga Bw Aljiran Mbwani (Kulia) akipokea cheti cha shukrani ya ushiriki na udhamini kutoka kwa Katibu Tawala wa mkoa wa Tanga Bi Pili Hassan ikiwa ni utambuzi wa mchango wa benki hiyo katika kufanikisha Maonesho ya nane ya biashara yaliyomalizika mwishoni mwa wiki kwenye viwanja vya Mwahako jijini Tanga.

Ahadi hiyo imetolewa na Meneja Maendeleo ya Biashara Benki ya NBC tawi la Tanga Bw Aljiran Mbwani wakati akielezea huduma za benki hiyo mbele ya Katibu Tawala Mkoa wa Tanga Bi Pili Hassani kwenye Maonesho ya nane ya biashara yaliyohitimishwa mwishoni mwa wiki kwenye viwanja vya Mwahako jijini Tanga.

Maonesho hayo yalihusisha wadau mbalimbali ikiwemo taasisi za kifedha, mamlaka na taasisi za serikali, wadau wa utalii, wakulima na wajasiriamali kutoka ndani na nje ya jiji hilo.

Aidha Mbwani alibainisha kuwa kwa kutambua umuhimu wa wajasiriamali na wakulima jijini humo benki hiyo imekuwa mstari wa mbele kushirikiana na makundi hayo kwa kutoa mafunzo ya ujasiriamali na kilimo biashara kabla ya kuwapatia mikopo.

“ Hata hivyo kwa jiji la Tanga ushirikiano tunaupata zaidi kutoka kwa wakulima wakubwa hususani wa mazao ya katani na viungo wakati tukiendelea kuwaamsha zaidi wafanyabiashara wadogo na wakulima wadogo. Uamshwaji huu unafanyika kupitia mafunzo ya biashara kwa wajasiriamali na elimu kuhusu mikopo sahihi tunayoitoa kwa wakulima.’’ Alisema

Alizitaja baadhi ya huduma mbalimbali mahususi kwa makundi hayo kuwa ni pamoja na akaunti za  NBC Shambani, Kua Nasi, akaunti ya malengo, akaunti ya Johari ambayo ni mahususi kwa ajili ya wanawake pamoja na huduma za mikopo.

Mbali na kushiriki maonesho hayo benki ya NBC ilikuwa ni moja ya wadhamini muhimu wa maonesho hayo yaliyofanyika kwa mafanikio makubwa ambapo yalivutia washiriki wengi zaidi huku pia ikishuhudiwa mamia ya wakazi wa jiji hilo wakijitokeza kutembelea maonesho hayo.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents