Waliofariki kwa tetemeko la ardhi Indonesia wafikia 268
Watu wapatao 268 wamekufa kutokana na maafa ya tetemeko la ardhi magharibi ya kisiwa cha Java nchini Indonesia. Wengi miongoni mwa waliokufa walikuwa watoto.
Maafisa wanaoshuhgulikia hali za dharura wamesema watu wengine zaidi ya 150 hawajulikani walipo, wakati waokoaji wanaendelea na harakati za kuwatafuta watu wanaohofiwa kufunikwa chini ya mabaki ya majengo yaliyoangamizwa.
Tetemeko hilo lililofikia kipimo cha 5.6 lilikumba jimbo la Indonesia lenye idadi kubwa ya watu kupita mengine yote.
Maafa hayo yamesababisha madhara makubwa kwenye mji wa Cianjur uliopo umbali wa kilomita 75 kusini mashariki ya mji mkuu, Jakarta.
Kijiji kimoja kimefunikwa kutokana na maporoko ya ardhi. Watu zaidi ya 1000 wamejeruhiwa na miundombinu kadhaa imeharibiwa.
Rais wa Indonesia Joko Widodo alikwenda kwenye mji huo wa maafa na ameahidi kuwalipa wahanga fidia. Pia ameahidi kuwa serikali yake itayajenga upya majengo yaliyoporomoka.