Wanajeshi Uingereza kuchukua nafasi ya wafanyakazi wanaogoma
Uingereza Jumapili imesema kwamba itatuma wanajeshi 1,200 kuchukua nafasi ya madereva wa magari ya kubeba wagonjwa pamoja na maafisa wa mpakani, wakati kuanza kwa mgomo wa wafanyakazi kutoka vyama tofauti vya wafanyakazi nchini humo, wiki moja kabla ya sherehe za Krismasi.
Wafanyakazi wa magari ya kubeba wagonjwa wanatarajiwa Jumatano wanajiunga na wauguzi, wafanyakazi wa reli, maafisa wa uhamiaji pamoja na wafanyakazi wa posta ambao wamepanga kushiriki kwenye mgomo wa kitaifa katika wiki zijazo.
Ripoti zimeongeza kusema kwamba wafanyakazi wanalalamikia kupanda kwa gharama ya maisha hasa kwenye bei za vyakula na nishati. Vyama vya wafanyakazi vinadai nyongeza ya mishahara kutokana na kushuka kwa thamani ya sarafu.
Serikali ya kikonsavative iliyoko madarakani imeonya kwamba thamani ya sarafu itashuka zaidi. Athari za janga la corona pamoja na uvamizi wa Russia nchini Ukraine vinaelezewa kuchangia kupanda kwa gharama za chakula na nishati.