Katika mji mkuu wa eneo la mashariki, Benghazi eneo ambalo ni kitovu cha uasi wa mwaka 2011 na kwenye mji mkuu wa Libya, Tripoli, maelfu ya waandamanaji waliingia mabarabarani kudai kurudishwa kwa huduma za umeme na kuzorota kwa hali ya maisha kwa jumla. Wengine walipeperusha bendera za kijani za utawala wa zamani wa rais aliyeondolewa madarakani na kishan kuuawa Muammar Gadhafi. Maandamano pia yalifanyika katika mji mwingine wa Misrata.
Utulivu ulionekana kurejea katika jiji la Tobruk jana Jumamosi, ingawa kulikuwa na miito kwenye mitandao ya kijamii wa kuhimiza maandamano zaidi.
Stephane Dujarric, msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema katibu mkuu ametoa wito kwa pande zote kujiepusha na vitendo vyovyote vinavyoweza kudhoofisha uthabiti nchini Libya na amewataka wahusika kushirikiana pamoja ili kuondokana na mkwamo wa kisiasa unaoendelea nchini humo.