Waziri Makamba aahidi kupambana na urasimu kwenye gesi
Serikali ya Tanzania leo imeanza mazungumzo rasmi na wawekezaji wa makampuni mawili kwa ajili ya uchakataji wa gesi asilia iliyogunduliwa baharini huko Kusini Mtwara.
Akizungumza na Waandishi wa habari Waziri wa Nishati, January Makamba amesema kwamba mradi huo wenye thamani ya Trilion 70 unatakiwa kukamilika mapema ili gesi hiyo ianze kuuzwa nje ya nchi na nyingine kwa matumizi ya hapa nchini.
Leo Novemba 8 akiwa Jijini Arusha, Waziri Makamba, amesema kwamba mazungumzo ya kukamilisha mradi huu yalikuwa yakisuasua na kupitia awamu hii chini ya Rais Samia Suluhu ameelekeza mazungumzo hayo yakamilike mapema.
Akizungumzia hatua alizopiga kwenye mradi huo Mh. Makamba, amesema
tayari wamefanikisha kuunda timu yenye ngazi tatu ikiwepo ya Uongozi, Majadiliano na Wataalamu ili kuhakikisha kwamba mazungumzo juu ya mradi huo hayakwami.
“Chini yangu kama Waziri wa Nishati tumeingia kwa spidi sana, nitalisimamia karibu sana ili kuondoa vikwazo vyote vilivyokua vikisababisha kusuasua tangu 2016. Na mpaka sasa tumeshaviondoa vikwazo vyote vya kirasimu. Tupo pazuri” Waziri Makamba.
Pamoja na hayo Mh. Makamba amesisitiza kuwa wamejipa muda usiopungua miezi 6 wa kufanya mazungumzo juu ya mradi huo ili kuhakikisha wanapata mkataba sahihi na wa uhakika ambao utakuwa una manufaa kwa wananchi wa Tanzania.
Akielezea baadhi ya fursa zitakazopatikana kwenye mradi huo, Waziri amesema kwamba mradi huo utakwenda kubadilisha maisha ya watanzania wengi na kuongeza kwamba zitazalishwa ajira zisizopungua 7000 zitakazodumu kwa miaka isiyopungua saba.
BY : Fatuma Muna