Mwalimu wa shule ya msingi ampachika mimba mwanafunzi wake
Mwalimu Daniel Saulo wa Shule ya Msingi Matui anashikiliwa na Jeshi la polisi kwa tuhuma za kumpa ujauzito mwanafunzi wake wa darasa la saba.
Akithibitisha taarifa hizo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Christopher Foime, amesema mtuhumiwa huyo tayari amekamatwa na yuko katika Kituo cha Polisi Matui kwa ajili ya upelelezi na uchunguzi zaidi.
“Kwa sasa mtuhumiwa tunamshikilia Kituo kidogo cha Polisi Matui, anaendelea na mahojiano, atafikishwa mahakamani wakati wote taratibu zitakapokamilika ili sheria ifuate mkondo wake,” amesema Kamanda Foime.
Kwa upande mwingine, Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Victoria Mushi, alikiri kukamatwa mwalimu huyo akisema tukio hilo ni la tatu kujitokeza shuleni hapo na kwamba hawezi kusema lolote kwa sasa.
“Nilikuwa Kanisani sikupokea mapema simu yako, kuhusu suala hili la mwalimu yupo Polisi kwa sasa siwezi kuzungumzia lolote, ingawa matukio haya yamekuwa yakijirudia ni tukio la tatu, kwahiyo bado siwezi kusema lolote kwa sasa ndugu yangu,” amesema Mwalimu Mushi.
Naye, Baba mzazi wa mtoto huyo, Isaka Maro alieleza masikitiko yake kwa Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Victoria Mushi kwa kuficha tukio hilo ingawa alilifahamu toka mwanzo baada ya shule kuwapima wanafunzi hao.
Chanzo : Mtanzania