Zaidi ya watu elfu 30 kufanya usaili wa nafasi 400 TRA
Zaidi ya Watanzania 30,000 wamejitokeza kufanya usaili katika kanda kumi zilizopo maeneo mbalimbali nchini, kwa ajili ya kuwania ajira 400 zilizotangazwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Usaili uliofanyika jana katika Uwanja vya Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu (DUCE) jijini Dar es salaam, mahali ambapo usaili mmoja ulikuwa ukiendelea, naibu katibu wa Sekretarieti ya Ajira, anayeshughulikia udhibiti wa ubora, Humphrey Mnyachi amezitaja kanda hizo kuwa ni pamoja na Dar es Salaam, Mtwara, Mbeya, Iringa, Mwanza, Arusha, Tabora, Dodoma, Morogoro na Zanzibar.
Mnyachi amesema usaili huo utafanyika kwa kuandika, kuzungumza na kwa vitendo kwa muda wa siku tatu kuanzia jana mpaka hadi tarehe ijumaa tarehe 1 septemba, 2017.
Mnyachi amesema usaili huo wa TRA unafanyika kwa kada saba ambazo ni forodha, wakusanyaji mapato, kodi, rasilimali watu, uhasibu na Tehama.
Akizungumzia hali nzima ya usaili Mnyachi amesema wamekutana na changamoto ya baadhi ya watahiniwa kutokuwa na vyeti vya elimu ya sekondari kwa madai walivipoteza na wengine kuchelewa kwenye vyumba vya usaili.
Hata hivyo, Mnyachi amesema matokeo ya wingi wa watu waliojitokeza kufanya usaili huo katika maeneo mbalimbali haimaanishi kuwa watu hawana ajira isipokuwa ni kwamba wengi wao wanafanya kazi kwenye taasisi binafsi na sasa wanatamani kupata ajira serikalini.
Chanzo:Mwanachi