Habari

Anayesakwa na TAKUKURU kwa zawadi ya mil. 10 ajisalimisha ‘Hizo hela saidieni jamii’

Aliyekuwa anatafutwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU), Godfrey Gugai, amejitokeza na kujisalimisha kwenye taasisi hiyo na kukanusha taarifa kuwa ametoroka nje ya nchi.


Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya TAKUKURU kutangaza donge nono la shilingi Milioni 10 kwa atakayefanikisha kukamatwa kwake.

Bw. Godfrey Gugai anatuhumiwa kujipatia mali nyingi kinyume na sheria ya Utumishi wa Umma ambapo taarifa iliyotolewa jana na Naibu Mkurugezi wa TAKUKURU, Brigedia Jenerali John Mbung’o ilidai ametoroka nchini.

Bw. Gugai amesema kuwa taarifa zilizotangazwa za kuwa anatafutwa zimemsikitisha kwani yeye yupo nchini na hajatoroka kwenda mahala popote kama ilivyotangazwa.

Nimesikitika kwa sababu kwa taasisi kama TAKUKURU, taasisi yenye dhamana ya uchunguzi, sikutegemea kiongozi mwenye dhamana aseme kwamba nimekimbilia Congo, kwa sababu taasisi kama hiyo yenye dhamana ilikuwa na wajibu wakuangalia kwenye mipaka kama kweli nimekwenda nje ya nchi.” amesema Godfrey Gugai .

Kuhusu tuhuma zilizotolewa dhidi yake amesema kuwa ameamua kufika makao makuu ya TAKUKURU ili suala hilo liweze kwenda Mahakamani kwa sababu mahakama ndio chombo pekee chenye kutoa haki.

Tuhuma zimetolewa lakini nimeambiwa ni suala la kimahakama ndio maana nimeamua mimi mwenyewe kufika makao makuu ya TAKUKURU ili suala hilo liende mahakamani na kwakuwa mahakama ndio chombo chenye kutoa haki itaamua. Naomba uueleze umma asije akatokea mtu yeyote kwamba amenitafuta mimi ili apate hilo donge nono, hilo donge nono ninashauri litumike kwenye huduma muhimu za kijamii, kama sekta ya Afya wazipeleke huko zisaidie wananchi kwenye jamii ambao wanahitaji huduma za Afya.“amesema Gugai.

Kwa upande mwingine, TAKUKURU wamethibitisha taarifa hizo za kujisalimisha kwa Bwana Gugai ambapo wamesema kwa sasa anashikiliwa na vyombo vya ulinzi na usalama.

Chanzo:ITV

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents