Maelfu ya watu waingia mtaani kuandamana
Maelfu ya watu wameandamana nchini Ufaransa katika vuguvugu lijulikanalo kama “yellow vest” wakipinga sera za kiuchumi za Rais wa taifa hilo, Emmanuel Macron.
Waandamanaji hao ambao walikuwa wamevalia vizibao vya njano waliandamana jana Jumamosi nchini kote, ikiwa ni miezi mitatu tangu vuguvugu hilo lianze.
Wizara ya mambo ya ndani ya Ufaransa, imesema waandamanaji wapatao 41,500 waliandamana kwa wikendi ya 14 mfululizo nchini kote. Idadi hiyo ikiwa ya chini ikilinganishwa na watu zaidi ya laki mbili waliokuwa wakiandamana mwanzoni mwa maandamano hayo ya kupinga sera za kiuchumi za Rais Emmanuel Macron.
Tayari Bunge la Umoja wa Ulaya siku ya Alhamisi ya wiki hii, lililaani matumizi ya polisi kutumia nguvu dhidi ya waandamanaji hao, hii ni baada ya mjadala kuzuka kuhusu polisi wa Ufaransa kutumia silaha za moto dhidi ya waandamanaji.