Mtoto wa siku 7 aliyeibiwa Songea na kuuzwa kwa Tsh 30,000/=, apatikana Moshi
Yametimia, mtoto Shazira Yahaya aliyeibiwa akiwa na wiki moja katika Kijiji cha Likalangiro Wilaya ya Songea Mjini mkoani Ruvuma, amepatikana katika Kijiji cha Kokirie Wilaya ya Moshi Vijijini mkoa wa Kilimanjaro, ambapo aliuzwa kwa Sh 30,000.
Taarifa za kupatikana kwake zimethibitishwa na Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Gemini Mushy, ambapo amesema mtoto huyo kwa sasa ana miezi mitano. Aliibiwa mnamo Septemba 26 mwaka 2018 na amepatikana Moshi vijijini Februari 18 mwaka huu.
Kamanda Mushy amesema baada ya jeshi hilo kupokea taarifa ya kupotea kwa mtoto huyo kutoka kwa mama mzazi, Amina Abdalah (17), upelelezi ulianza hadi kufikia Februari 18 mtoto alipopatikana.
Mushy akitaja mtuhumiwa aliyehusika kumuiba mtoto huyo na kisha kwenda kumuuza, kuwa ni Abrahamu Kilewa (20) mkazi wa kijiji cha Mahanje katika Halmashauri ya Madaba na alienda kumuuza kwa Anosiata Luambano (36) ambaye ni mfanyabiashara na ni mkazi wa Marangu Moshi ambaye anadaiwa alimnunua kwa TSh 30,000.
“Mtoto huyo aliuzwa kwa Sh 30,000 akiwa ana umri wa siku saba, tumepata baada upelelezi mkubwa ulifanywa na Askari F.2229D/CPL Victor ambaye alijituma kwa kujitolea uhai wake kwenda kumuokoa mtoto huyo,”. amesema kamanda Mushy.
Chanzo: http://mtanzania.co.tz/mtoto-aliyeibia-songea-apatikana-moshi-alikouzwa-kwa-sh-30000/