RPC Dodoma atangaza vita na watu wanaouza mafuta kiholela, 45 waingia kwenye anga zake
Jeshi la Polisi mkoani Dodoma limetangaza msako mkali wa kuwakamata watu wanaouza mafuta kinyume cha taratibu, Hii ni baada ya watu 45 kukamatwa na Jeshi hilo wakifanya biashara hiyo kando kando mwa barabara.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano Septemba 18, 2019 Jijini Dodoma, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema kuwa tayari wamefanikiwa kukamata lita 4,445.
Kamanda Muroto amesema biashara hiyo ni hatari kwa kuwa inaweza kusababisha moto kwenye makazi ya watu. Lita hizo zilizokamatwa ni za mafuta ya Petroli na Dizeli .
Muroto amesema watuhumiwa hao wamekamatwa baada ya jeshi la polisi kufanya msako kwenye wilaya zake zote za mkoa wa Dodoma kwa kushirikiana na wakuu wa polisi wa wilaya na kufanikisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao.
Kwa upande mwingine, Kamanda Muroto amesema jeshi la polisi mkoani humo, Litaanza kuwachukulia hatua wenyeviti wa serikali za mitaa watakaoshindwa kuwabainisha wale wote wanaojihusisha na biashara hiyo.