SIMANZI: Mama aporwa mtoto wake na Simba, Yadaiwa aliingia ndani na kuwakuta wakiwa wamelala kitandani
Mtoto mmoja wa miaka 6 aliyetambulika kwa jina la Kangwa Manuga ameuawa na Simba, Baada ya kuchukuliwa kitandani akiwa amelala na mama yake mzazi katika Kijiji cha Sitalike wilayani Mpanda, mkoani Katavi.
Akithibitisha taarifa hizo mbele ya waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Benjamin Kuzaga, amesema tukio limetokea mwishoni mwa wiki iliyopita majira ya saa 4 usiku akiwa amelala na mama yake nyumbani kwao.
“Walikuwa wanaishi nyumba ambayo haikuwa na mlango imara, huyu mtoto siku zote yuko na wazazi wake, siku ya tukio baba hakuwapo nyumbani. Ule udhaifu wa mlango ulichangia mnyama huyu kuingia ndani kirahisi,” ameeleza Kamanda Kuzaga.
Kamanda Kuzaga amesema Simba huyo aliwaacha ng’ombe ambao walikuwa ndani ya nyumba hiyo ambayo ina muonekano kama kibanda na kumchukua mtoto huyo..
“Simba aliingia ndani na kumchukua mtoto huyo, kisha kutoka naye nje na kumuacha mama yake akiangua kilio na kupiga makelele,” Amesema Kamanda Kuzoga.
Aidha, Kamanda Kuzoga amesema kuwa mama huyo alianza jitihada za kumuokoa mtoto wake mdomoni mwa Simba kwa kumrushia kuni zilizokuwa zikiwawaka moto, huku akipiga yowe kuomba msaada kwa majirani.
Hata hivyo, Licha ya jitihada zote hizo, Simba alifanikiwa kukimbia na mtoto huyo vichakani, Ambapo wanakijiji baadae walifika eneo la tukio na walikuta mtoto huyo tayari ameliwa na Simba huyo ambaye hawakuweza kumwona.
Chanzo: Mtanzania