Habari

Waziri wa Rais Magufuli akiri kuwa Wizara yake ina ‘udhaifu’, Asema kuna watu wanashindwa kutekeleza majukumu yao

Waziri wa Viwanda, Biashara, Mhe. Joseph Kakunda, amesema wizara yake ina udhaifu mkubwa katika kusimamia utekelezaji wa sera zilizo chini ya uratibu wake kutokana na kukosa uwakilishi wa kitaalamu kwa sekta ya viwanda kwenye sekretarieti za mikoa na halmashauri.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli mwaka jana wakati akimuapisha Joseph Kakunda kuwa Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Aprili 16, 2019 jijini Dar es Salaam, Waziri huyo amesema ukosefu wa maofisa wa viwanda katika mikoa na halmashauri kumesababisha udhaifu kwenye upatikanaji wa taarifa sahihi kuhusu usajili wa viwanda na leseni za viwanda, uwezo wa viwanda wa uzalishaji, idadi ya wafanyakazi, shehena zilizouzwa ndani ya nchi, zilizouzwa nje ya nchi na zilizo kwenye maghala.

Napenda nikiri wizara yangu ina udhaifu mkubwa katika kusimamia utekelezaji wa sera zilizo chini ya uratibu wake,” amesema Waziri Kakunda na kuongeza.

“Ni vizuri utaratibu wa utekelezaji wa majukumu ikiwamo takwimu za viwanda uanzie kwenye halmashauri, mkoa ndipo uje makao makuu ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kuratibiwa na Tamisemi,” .

Kwa upande mwingine, Waziri Kakunda ameagiza Shirika la Viwango nchini (TBS), Wakala wa Vipimo (WMA) na Tume ya Ushindani (FCC), kufanya mapitio ya kanuni ili kupunguza viwango vya tozo wanazowatoza wenye viwanda na wafanyabiashara na kuleta marekebisho kabla ya Juni 30, mwaka huu.
Aidha, ameagiza WMA kufanya ukaguzi wa uzalishaji wa bidhaa hasa katika viwanda vya nondo, mabati, marumaru, misumari na mabomba ya chuma ili kuangalia uzingatiwaji wa vipimo na kuwapa elimu kuhusu vipimo sahihi wenye viwanda hivyo.
Nimeagiza WMA wafanye ukaguzi wa uzalishaji wa bidhaa ili bidhaa zinazotoka Tanzania ziendelee kukubalika kuwa bora kwenye masoko ya nchi za Afrika Mashariki, SADC, Afrika na nje ya Bara la Afrika,” Kakunda alisema.

Chanzo: Nipashe

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents