Askofu apongeza zoezi la serikali kuhakiki vyeti
Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo Kikuu cha Iringa, Askofu Dk Owdenburg Mdegella amepongeza uamuzi wa serikali ya awamu ya tano ya uhakiki wa vyeti vya watumishi wake, huku akisema utasaidia kumaliza hali mbaya ya ongezeko la vyeti bandia.
Askofu Dk Owdenburg Mdegella
Akizungumza kwenye mahafali ya 19 ya chuo hicho, Askofu Dk Mdegella alisema uhakiki huo una mafanikio, kwani unapembua chuya kutoka kwenye mchele safi.
“Kwa kupembua chuya, serikali inataka kubaki na wajuzi wenye vyeti halali katika utumishi wake wa umma, jambo linalopaswa kupongezwa,” alisema Dk Mdegella.
“Watu hawa wanaweza kuwa na haki na maslahi yanayofanana, lakini tofauti yao ni kwamba yule aliyepata vyeti bandia vyenye ufaulu wa hali ya juu anakuwa hana ujuzi wa kazi aliyopewa, jambo lililokuwa likirudisha nyuma maendeleo ya taasisi nyingi na nchi kwa ujumla,” alisema.
Aidha alisema uhakiki wa vyeti unapaswa kuungwa mkono na wadau wote na kuna haja usiishie kwa watumishi wa umma, bali uende hadi kwa watumishi wa sekta binafsi.
BY: EMMY MWAIPOPO
CHANZO: HABARI LEO