Habari

Mh. Shonza aitaka Bodi ya Filamu kufanya utafiti kuona takwimu za mapato ya sekta hiyo

Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo, Juliana Shonza ameitaka Bodi ya Filamu Tanzania kufanya utafiti na kukusanya takwimu sahihi za mapato yatokanayo na sekta ya filamu nchini ili kuweza kubaini sekta hiyo inavochangia katika pato la taifa.

Mhe. Shonza ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam alipofanya ziara katika Ofisi za Bodi ya Filamu Tanzania na kuzungumza na watendaji wa bodi hiyo huku akiwataka kuweka mifumo ambayo itasaidia wasanii kuinua, kuboresha na kuendeleza tasnia ya filamu nchini.

Shonza ameitaka bodi ya filamu kuhakikisha kuwa inasimamia maadili katika filamu pamoja na ubora wa filamu ili filamu zinazotengenezwa nchini ziwe na kiwango kitakachowavutia wadau wa filamu ndani na nje ya nchi kupenda filamu zetu.

Mhe. Shonza amesema kuwa katika kukuza vipaji Bodi ya filamu ifanye jitihada za kuwafikia na kutoa elimu kwa wanatasnia ya filamu waliopo mikoani kwani huko nako kuna wasanii wenye uwezo wa hali ya juu lakini vipaji vyao havionekani kutokana na kutofikiwa kwa wakati.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji Bodi ya Filamu Bibi. Joyce Fissoo amemhakikishia Mhe. Naibu Waziri kuwa Bodi ya Filamu itaendelea kukaza kamba na kuhakikisha kuwa haioni haya katika kutekeleza majukumu yake kwa mujibu ya sheria na kanuni zilizopo.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents