Polisi ahukumiwa kifo Kenya
KENYA Mahakama kuu nchini humo imemhukumu kifo afisa wa Polisi, Fredrick Ole Leliman kwa mauaji ya wakili Willie Kimani na wengine wawili yaliyotokea mwaka 2016.
Maiti za watatu hao zilipatikana zimeshindiliwa kwenye mifuko ya plastiki na kutupwa mtoni kaunti ya Machakos.
Hukumu ya kifo ilitekelezwa kwa mara ya mwisho kiasi cha miaka 30 iliyopita japo bado adhabu hiyo inaendelea kutolewa.
Mnamo Ijumaa katika mahakama kuu nchini Kenya, Jaji Jessie Lessit ambaye sasa ni wa mahakama ya rufaa, aliwapata na hatia ya mauaji na kumhukumu kifo afisa wa polisi Fredrick Ole Leliman kwa mauaji ya wakili huyo na wengine wawili ya mwaka 2016.
Afisa wa polisi Stephen Cheburet amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela, mwenzake Sylvia Wanjiku miaka 24 jela na Peter Ngugi aliyekuwa mdakizi atafungwa miaka 20 jela.
Watatu hao walitiwa hatiani mwezi Julai mwaka uliopita wa 2022.