Breaking: Nahodha wa Simba SC ‘Jonas Mkude’ apata ajali mbaya ya gari
Nahodha wa Klabu ya Simba SC, Jonas Mkude amepata ajali baada ya gari waliokuwa wakisafiri nalo kupinduka katika eneo la Dumila mkoani Morogoro wakati wakirejea jijini Dar es salaam wakitokea mjini Dodoma.
Ajali hiyo iliyohusisha gari yenye namba za usajili T 834 BLZ, Toyota VX imetokea baada ya tairi la nyuma ya gari hiyo kupasuka na kusababisha majeruhi wawili ambapo wamewahishwa kwenye hospitali ya rufaa mkoani Morogoro kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
“Kiungo Jonas Mkude apata ajali ya gari wakati akirudi jijini Dar es Salaam.Amepatiwa huduma ya kwanza na sasa anapelekwa Dar es Salaam kwa matibabu zaidi. Ajali hiyo imetokea baada ya tairi ya gari ya nyuma kupasuka. Majeruhi wengine wawili waliokuwemo kwenye gari hiyo wamewahishwa kwenye hospital ya Morogoro.“,Imeandika Klabu ya Simba kwenye ukurasa wake wa Instagram.
Kupitia ukurasa wa Instagram wa klabu hiyo Simba wamethibitisha kifo cha mtu mmoja ambaye alikuwa ni shabiki wao “Shabiki mkubwa wa klabu ya Simba afariki kwenye ajali ya gari,Katika ajali ya gari ambamo kiungo Jonas Mkude alikuwemo, shabiki, mwanachama na mpenzi mkubwa wa klabu ya Simba Shose amefariki dunia baada ya kupata majeraha makubwa kutokana na ajali hiyo.”
Klabu ya Simba ilikuwa mkoani Dodoma tangia juzi ikijiandaa kwa mchezo wa Fainali ya kombe la Shirikisho kati yake na Mbao FC ambapo Simba ilishinda kombe hilo kwa kuichapa Mbao FC goli 2-1.