Habari

Maafisa habari wa serikali 300 kukutana Arusha

Maafisa Habari na Mawasiliano 300 kutoka katika Taasisi na Idara za Serikali, Halmashauri, Majiji na Mikoa yote ya Tanzania wanatarajia kukutana Jijini Arusha katika mkutano wa mwaka wa Chama cha Maafisa Mawasiliano Serikali kuanzia Machi 12 hadi 16 mwaka huu.

Mkurugenzi wa Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi alisema hayo Jijini Arusha alipotembelea radio za Sunrise pamoja na Triple A FM za mkoani Arusha kwa nia ya kuwaalika katika mkutano huo pamoja na kujua changamoto wanazopitia.

“Mkutano wa Maafisa Mawasiliano Serikalini unaotarajia kufanyika mkoani hapa ni fursa kwa vyombo vya habari vya mkoa huu, kukutana na Maafisa Habari na Mawasiliano kutoka taasisi zote za Serikali ambao ndio wenye taarifa za taasisi zao. Hivyo ni vyema waandishi wa habari mkashiriki kwa wingi kwa ajili ya kupata taarifa za taasisi zao pamoja na mawasiliano yao,”alisema Dkt. Abbasi.

Aliviarika vyombo vya habari kutumia fursa ya mkutano wa huo kufanya mahojiano na Maafisa Mawasiliano hao ambao wametoka sekta mbalimbali za Serikali kwa ajili ya kutolea ufafanuzi masuala yote yanayohusu miradi na utekelezaji wa ahadi za Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Maafisa Mawasiliano Serikalini (TAGCO) Pascal Shelutete amesema lengo la mkutano huo ni kuwanoa Maafisa Habari na Mawasiliano wa Serikali kuhakikisha wanatoa taarifa kwa wananchi juu ya shughuli zote zinazofanywa na Serikali katika Taasisi zao.

Ameongeza kuwa, Maafisa hao watapatiwa mafunzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutoa ujumbe kwa njia ya picha pamoja na namna ya kutumia mawasiliano ya kimkakati katika ujenzi wa Tanzania ya viwanda.

Nae Katibu Mwenezi wa TAGCO, Dkt. Cosmas Mwaisobwa amesema chama hicho kinatarajia mabadiliko makubwa kwa Maafisa hao katika kikao cha mwaka huu, vile vile wananchi wategemee kupata taarifa zote za utekelezaji wa ahadi za Serikali kupitia Maafisa hao.

Mkutano Mkuu wa Maafisa Habari na Mawasiliano Serikali unatarajiwa kufunguliwa Machi 12 mwaka huu na Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe na kufungwa Machi 16 mwaka huu na Waziri Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. Selemani Jafo. Mkutano huo utaoneshwa mbashara kupitia televisheni ya mtandao ya MAELEZO inayopatikana “YOUTUBE”.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents