Tuhuma za kauli za kichochezi zamrudisha Mhe Lissu rumande
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) na Mbunge wa Singida Mashariki, Mhe Tundu Lissu amefikishwa katika Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam na kusomewa mashtaka ya kutoa lugha ya uchochezi.
Akisomewa mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri leo Jumatatu, Julai 24, mahakama imeeleza kuwa Lissu ametoa lugha ya uchochezi dhidi ya Serikali Julai 17 akiwa maeneo ya Ufipa, Kinondoni jijini Dar es salaam.
Imedaiwa kuwa maneno hayo yalikuwa na lengo ya kuleta chuki dhidi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alipotakiwa kukubali ama kukataa makosa hayo mbele ya Hakimu Mashauri, Lissu amesema kusema kweli haijawahi kuwa kosa la jinai kwa maneno aliyotamka.
Mhe Lissu amenyimwa dhamana na kurudishwa rumande mpaka Tar 27 Julai kesi yake itakaposikilizwa tena.