Habari

Tumieni malighafi za nchini katika viwanda vyenu – Mh. Samia Suluhu

Serikali imezitaka nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki kutumia malighafi zinazopatikana katika nchi hizo kwa ajili ya viwanda badala ya kuagiza kutoka nje.

 

Rai hiyo imetolewa jijini Dar es salaam na makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan wakati akifungua Mkutano wa Pili wa Biashara na Ujasiriamali ya Afrika Mashariki.

“Ndoto yetu ya uchumi wa viwanda sio kuhamishia viwanda vya nje hapa nchini bali ni kuwa wabunifu na kujenga viwanda vyetu wenyewe,”amesema Samia.

Amesema ujenzi wa uchumi wa viwanda uendane na kufanya kilimo chenye tija ambacho kinalenga kuwaondolea umaskini wananchi.

“Wakulima wetu hawana uhakika na soko la mazao yao kwani wanapopata mazao kwa wingi, bei inashuka, wakati wa ukame mazao yanaharibika, hivyo kwao nyakati zote ni taabu,” amesema Mhe. Samia.

Makamu wa Rais amewataka wakulima waongeze thamani ya mazao yao badala ya kuuza mazao ghafi. Kwa kufanya hivyo watajiongezea kipato na kuondokana na umaskini, aliongeza Samia.

Uanzishwaji wa viwanda katika Jumuiya ya Afrika mashariki utasaidia katika kuinua kilimo kwani mazao hayo yatapata uhakika wa soka kwenye viwanda hivyo.

Amezitaka nchi hizo kutengeneza ajira hasa kwa vijana ambao takwimu zinaonyesha kuwa ndio wengi, hivyo ni muhimu kuwapa kipaumbele.

Serikali na sekta binafsi zimetakiwa kufanya juhudi za makusudi kuanzisha viwanda ambavyo vitaongeza ajira na kuifanya Tanzania kuwa na uchumi wa viwanda.

Aidha, Mhe. Samia amezitaka nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kudumisha amani kwani bila amani uwekezaji katika viwanda na maeneo mengine hauwezekeni.

Amani ni bidhaa adimu ambayo inapatikana kwa gharama, hivyo siyo ya kuchezea bali ni ya kulindwa, aliongeza Mhe. Samia.

Huu ni Mkutano wa Pili ambao unajumuisha washiriki kutoka, Kenya, Burundi, Rwanda, Uganda na wenyeji Tanzania. Katika Mkutano huo yanafanyika maonyesho ya wajasiriamali kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashiriki.

Imetolewa na MAELEZO

 

 

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents