Ruvu Shooting yawatema wachezaji 10
Klabu ya Soka ya Ruvu Shooting imewaacha wachezaji wake kumi kutokana na sababu mbalimbali, huku ikiweka bayana kuanza mchakato wa kusajili wachezaji wengine wa pya.
Kikosi cha timu ya Ruvu Shooting kikitoka Uwanjani
Uongozi wa timu hiyo ulikutana chini ya mwenyekiti wake Kanali wa Jeshi, Mkuu wa Kikosi cha Jeshi (CO) 832, Ruvu JKT Charles Mbuge, kujadili taarifa ya kocha, Malale Hamsini baada ya msimu wa 2016/17 kumalizika.
Kutokana na mapendekezo ya kocha huyo, uongozi wa timu hiyo umeamua kuachana na wachezaji 10 wakiwamo kipa Elias Emanuel, Ismail Mgunda, Richard Peter, Claide Luita, Amour Bakari na Alex Sety.
Ofisa habari wa klabu hiyo, Masau Bwire amesema hakuna mchezaji muhimu aliyeachwa na wengi wao ni wale ambao hawakuwa na nafasi ya kutosha kwenye kikosi hicho ambacho kilimaliza Ligi kikiwa nafasi ya saba.
“Ukiangalia huyo kipa, Elias alicheza mchezo mmoja pekee dhidi ya Mbao Fc na alifungwa mabao manne, Ismail yeye alicheza michezo minne lakini alitoroka kambini hivyo ameondoshwa kwenye timu pamoja na wengineo.
“Ila kikubwa ni kutaka kukiboresha kikosi ili kwa msimu ujao kiwe na kasi zaidi tofauti na msimu huu ambao umemalizika, wachezaji tisa wanaotakiwa kusajiliwa ni beki wa kati mmoja, viungo wa pembeni wawili, viungo wakabaji wawili, beki wa kulia mmoja na washambuliaji watatu.” alisema Masau.
BY HAMZA FUMO