Afande adai nyimbo za mipasho sio dili, awataka wasanii wa Hip Hop kuimba nyimbo za kuijenga jamii
Msanii wa muziki wa Hip Hop kutoka Morogoro, Afande Sele amesema wasanii kujibishana kwenye nyimbo sio jambo la msingi kwani wanatakiwa waandae kazi ambazo zitaijenga jamii na kuleta tija kwa taifa.
Akizungumza katika kipindi cha Planet Bongo cha East Africa Radio Alhamisi hii, Afande aliuzungumzia wimbo wa Nay ‘Shika adabu yako’ na kutoa maoni yake juu ya wimbo huo kutokana na kuzungumzia watu mbalimbali.
“Nay kaimba kitu anachokiamini yeye na anachokiona yeye na ile ndio style yake ya muziki na hivyo inapotokea wewe unaanza kujibizana nae unakuwa ni wivu tu, husda kwa sababu yale ni mawazo yake yeye na ile ndio style yake ya muziki ambayo imemtoa toka ameanza game, mimi nawashauri kuwa hawana sababu ya kujibu kwa vile nyimbo yenyewe tayari imeshafungiwa na imeonekana na mapungufu mengi, mimi nadhani waache kama ilivyo waje na style nyingine muziki uendelee mbele,” alisema Afande Sele
Aidha, Afande amewataka wasanii kuacha kuimba nyimbo za kubishana kwani kuna vitu vingi vya kuimba ambavyo vitaleta tija kwa watanzania.
“Ningependa kuwashauri wasanii kipindi hiki waimbe vitu vya msingi ili wamsaidie Rais Magufuli kuongoza nchi na mambo ya kujibizana wamuachie Isha Mashauzi na Hadija Kopa kwani ndio kazi yao” alisema Afande.