Balozi wa Redd’s 2008 arudisha Taji
Mshindi wa taji la Balozi wa Redd’s katika mashindano ya Miss Tanzania mwaka huu, Angela Lubala amevua taji hilo na kurudisha kwa waandaaji
Pichani ni Meneja wa kinywaji cha Redds George Kavishe alipokuwa akimtambulisha balozi mpya wa kinywaji hicho,Angela Lubala ,kati ni balozi wa kinywaji cha redds aliyemaliza muda wake Victoria Martin
Mshindi wa taji la Balozi wa Redd’s katika mashindano ya Miss Tanzania mwaka huu, Angela Lubala amevua taji hilo na kurudisha kwa waandaaji.
Angela alisema amechukua uamuzi huo kutokana na imani yake ya dini ya Kikristo, ambapo yeye anaabudu kanisa liitwalo World Alive International Outreach lililopo Sinza, jijni Dar.
Alisema amefikia uamuzi huo bila kushawishiwa na mtu na anaona halitakuwa jambo la busara kuendelea kuwa Balozi wa kinywaji cha Redd’s, wakati imani ya dini yake haimruhusu
“Nachukua fursa hii kuiambia jamii kuwa kutokana na imani yangu katika Yesu Kristo, sitaweza kuwakilisha Redd’s kama Redd’s Fashion Ambassador 2008.
“Kwa kuwa mimi si mbinafsi, narudisha taji hili na zawadi zake zote kwa Redd’s, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Vodacom, Lino na Redd’s kwa uelewa juu ya uamuzi wangu huu”, alisema.
Vodacom ndio wadhamini wakuu wa Miss Tanzania. Angela ambaye pia ni Miss Temeke 2008, alisema zawadi anayorudisha ni fedha sh. Milioni 2.5.
Alipoulizwa kama hakujua wakati anashiriki mashindano hayo tangu mwanzo kama kuna jambo kama hilo, alisisitiza kuwa suala la kuwa Balozi wa kinywaji hicho haliendani na imani yake.