Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sana na Michezo Bw. Gerson Msigwa ameikabidhi timu ya Twiga Stars kitita cha Sh. Milioni 10 zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia ushindi waliopata dhidi ya timu ya Ivory Coast uliowawezesha kufuzu michuano ya WAFCON 2024.
Akikabidhi fedha hizo, Katibu Mkuu Bw. Msigwa amesema wachezaji hao wanafanya kazi kubwa ya kuiwakilisha nchi Kimataifa na Serikali ipo pamoja nao kwa kuwa wanaitangaza na kuipigania nchi yao.
“Mnapokuwa uwanjani katika mechi za kimataifa mnakuwa mmebeba matumaini ya watanzania, katika mechi zote mlizocheza tumeona dhamira mliyonayo kwa nchi yenu, Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anawapongeza sana, anafurahi sana anapowaona mnacheza uwanjani, anafurahi sana mnapopata matokeo mazuri katika mechi zetu” Katibu Mkuu Bw. Msigwa.