Burudani

Mambo 5 yanayomfanya Ruge kuwa na sifa ya ‘mkombozi wa BongoFleva’ (Video)

Ruge Mutahaba aka Scofield mtu ambaye amekuwa na mchango mkubwa kwenye muziki wa BongoFleva. Sio mbaya kumkosoa kama kuna sehemu aliteleza kama binadamu, mnyonge mnyongeni lakini haki yake apewe.

Ruge alianza kujulikana rasmi kwenye tasnia ya burudani baada ya kuanza kufanya kazi kama Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji wa Clouds Media Group, na baadaye kwenye Tamasha kubwa la muziki la Fiesta, Nyumba ya Kukuza Vipaji Tanzania THT, Semina za Fursa pamoja na mambo mengine mengi ambayo ameyafanya nyuma ya pazia. Haya ni mambo 5 ambayo ameyafanya Ruge na kuchangia ukuaji wa Mukizi wa BongoFleva Tanzania.

1. RUGE AMETENGENEZA MFUMO WA MUZIKI TANZANIA.

Huyu ni mmoja kati ya watu muhimu kwenye tasnia ya muziki nchini Tanzania, amefungua njia kwa wasanii wengi, amesaidia kujenga mifumo ya muziki pamoja na mazingira rafiki kwa ukuaji wa muziki wa BongoFleva. Kupitia Tamasha la Fiesta ambalo ndio kubwa kwa sasa nchini Tanzania, alitoa fursa kwa wasanii kuonyesha uwezo wao, alionyesha kitu tofauti katika maandalizi ya show zake kuanzia perfomance za wasanii, light, stage pamoja na mambo mengine mengi. Mafanikio ya tamasha hilo bila shaka ndio matunda ya matamasha mengine mengi yaliozaliwa miaka hii.

Pia Ruge aliweza kuwatengeneza vijana wengi na kuwaingiza katika biashara ya muziki. Alimtoa Babu Tale katika shughuli zake na kumuingiza kwenye tasnia ya muziki, na leo hii Tale ni mmoja kati ya mameneja wanao msimamia msanii Diamond Platnumz ambaye anamiliki label ya WCB.

………………..MANENO YA BABU TALE……………………..

“Mimi nilikua nafanya kazi kwenye kampuni ya miito ya simu na nilikua nalipwa milioni 1 kwa mwezi na kwa kuwa sina elimu basi niliona kama dodo mperani. But huyu bwana (Ruge) alikuja akaniuliza hivi unazani unafanana na hii pesa unayolipwa?. Mi nikahisi ananionea gere, basi alinikazia mwezi mzima na kuniambia rudi mtaani kasaidie mtaa na pesa utapata uko zaidi ya hii nikambishia then akajitolea kuwa atakua ananipa pesa bila hata ya kumfanyia kazi but nirudi kitaani hapo nikakubali nikaingia mtaani nikakomaa mpaka leo nimepata tobo naendesha maisha yangu na timu ya masela kibao wanaenda chooni kwa ajili yangu. Mungu akuweke boss leo umezaliwa na sina zawadi ya kukupa zaidi ya madua. Happy birthday Ruge”

Ruge amekuwa akitajwa na baadhi ya wadau kwamba yeye ndiye alimfungulia njia Diamond Platnumz mpaka kupatikana kwa kolabo ya Number One na Davido.

2. RUGE + CLOUDS KATIKA MAPINDUZI YA MUZIKI WA BONGOFLEVA

Clouds Media ni kituo cha kwanza cha redio nchini Tanzania kujikita zaidi kusupport muziki wa BongoFleva kwa 100%. Mkurugenzi wa Clouds Media Group, Joseph Kusaga pamoja na Ruge ambaye ni Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji wa Clouds Media Group walikuwa na lengo la pamoja la kuusupport muziki nzuri wa BongoFleva pamoja na kuandaa matamasha ya muziki huo. Ni kweli zipo redio nyingine ambazo zilikuwa kipindi hicho lakini Clouds walikuwa vinara wa kucheza nyimbo za vijana zaidi ambazo zilipendwa na wengi zaidi na kuufanya muziki wa BongoFleva kukuwa kwa kazi zaidi nchini Tanzania.

Ruge alikuwa ndio kila kitu Clouds kwa lugha za mtaani ‘kichwa’ ndio maana bifu nyingi na wasanii alikuwa akipambana nazo mpaka mwishoni na kuibuka mshindi. Akiwa kazini alikuwa ana project nyingi ambazo zilikuwa zikitoa fursa kwa wasanii wengi pamoja na vijana.

3. KUVUMBUA VIPAJI KUPITIA THT, DEAL NYINGI ZA SHOW, KAMPENI ZILIVYOWAPA FURSA WASANII NA KUBADILI MAISHA YAO.

Tanzania House Talents THT ni moja kati ya vituo vya kuzalishia vipaji vya muziki nchini Tanzania vilivyozalisha wasanii wengi sana. Kati ya 70% ya wasanii ambao tunawaona kwenye tasnia hii wamepitia kwenye kituo hicho au kusaidiwa kwa namna moja na kitengo hicho cha muziki, wasanii waliopita mikoni mwana THT ni pamoja na Barnaba Classic, Amini, Linah, Ditto, Mwasiti pamoja na wasanii wengine wengi.

Tukiachana na Tamasha la Fiesta ambalo linamchango mkubwa kwa wasanii wengi, Ruge alikuwa mmoja kati ya wadau muhimu wa muziki ambaye anaandaa kampeni nyingi kupitia THT ambazo zimezalisha fursa kwa wasanii wengi. Kampeni nyingi za serikali ambazo zilikuwa zinahitaji wasanii basi Ruge lazima atahusishwa na yeye Hutoa fursa kwa wasanii wa BongoFleva na BongoMovie.

4. RUGE NI FUNDI WA KUVUMBUA VIPAJI MBALIMBALI NA KIBADILI MIND SET ZA VIJANA.

Tukiachana na kuvumbua vipaji vya wasanii wa muziki, Nikki wa Pili ambaye ni msanii wa hip hop wa Kundi la Weusi, amekuwa akizungumza mara kwa mara kwamba anamshukuru sana Ruge Mutahaba kwa kutambua kipaji chake na kumpatia nafasi kwenye semina ya fursa kama mzungumzaji.

…………………………………………….MANENO YA NIKKI WA PILI………………………………………………

“My story na Ruge Mutahaba Muda wa kipindi kirefu sana katika maisha yangu ya shule nilikuwa naamini mimi ni mtu wa kukaa nyuma, nisiye na uwezo wa kuzungumza mbele za watu, sikuwa nanyoosha mkono darasani hata kama najua jibu, niliosoma nao chuo wanajua nilivyo kuwa natoroka presentations….Siku moja niliongea dakika mbili mbele ya watu….akaniona mtu anaitwa Ruge Mutahaba….jioni akaniita tukaaka tukapiga story….baada ya kama lisaa la kupiga story akaniambia…wewe unauwezo mkubwa wa kupanga mawazo, kujenga hoja lakini pia kueleza jambo kirahisi na kuumba taswira ….akaniambia wewe ni public speaker mzuri…..akaanza kunipa nafasi ya kuzungumza mbele za watu nilikuwa naona na kosea lakini kila niliposhuka alikuwa anaiambia umefanya vizuri sana ongeza hichi na hichi……….leo nimekuwa naalikwa vyuoni, kwenye makongamano, semina,taasisi, kampeni mpaka makanisani, kama mzungumzaji au mtoa mada……na hata mitandaoni huwa naandika mawazo yangu bila woga…….ingekuwaje nisingekutana na Ruge Mutahaba…….Mungu akupe wepesi urudi katika uzima wako..RG,” aliandika Nikki wa Pili.

5. RUGE NI MPENDA MUZIKI MZURI NA ANASIMAMIA ANACHOKIAMINI

Tasnia ya muziki wa BongoFleva bado inawahitaji watu kama Ruge, Kwani bosi huyo wa Clouds siku zote alikuwa akisisitiza muziki mzuri ndio kila kitu na kama unampelekea nyimbo mbaya basi atakwambia hii hapana. Ni watu wachache sana kwenye tasnia hii wenye uthubutu na kupembua mabaya na mazuri bila kuogopa kutengeneza chuki.

Mazingira hatarishi kwa vipaji tunalazimika kumuombea sana Ruge arudi kwenye afya yake. Mtu anayesimamia vipaji halisi miaka nenda rudi. Muda mfupi akiwa kitandani huku vipaji halisi vinatengwa tukiaminishwa kwenye mvuto wa sura na maumbo. Kwenye muziki huu Ruge atabaki kama mkombozi wa kweli aliyefungua njia na fursa kwa wasanii wengi Tanzania na tasnia ya muziki kwa ujumla.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents