Mshambuliaji ‘hatari’ wa Serengeti Boys azitolea nje Simba na Yanga
Mshambuliaji hatari wa Timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17 Serengeti Boys, Yohana Nkomola amegoma kujiunga na vilabu vikubwa vya ndani ya Tanzania zikiwemo Simba na Yanga, na kuweka wazi kuwa mpango wake ni kucheza soka nje ya Tanzania.
Nkomola ambaye ni zao la Kituo cha Kuzalisha Vipaji cha (Azam FC Academy), amesema mipango yake ya kucheza soka nje ya Tanzania bado ipo pale pale huku akiahidi kuwa hata kama ikikwama hatakuwa tayari kujiunga na klabu yoyote nchini ili kulinda kiwango chake kikishuke.
Akizungumzia kuhusu majaribio aliyokwenda kuyafanya katika klabu ya Etoile Du Sahel nchini Tunisia, Nkomola amesema majibu ni mazuri na anachosubiri makubaliano kati ya timu hiyo na wakala wake.
“Kuhusu majaribio yangu, nilishajibiwa kuwa nimefaulu, na timu ile imenipenda, hapa nilipo nasubiri kuitwa tu kwa ajili ya mkataba, sijui wamefikia hatua gani maana wanazungumza na wakala wangu,” alisema Nkomola kwenye mahojiano yake na Azam TV.
Hata hivyo amesema timu kubwa nchini zimekuwa zikimnyemelea zikiwemo Simba na Yanga lakini amezigomea huku akikanusha taarifa za kupata timu nchini Afrika Kusini pamoja na wachezaji wengine wa Serengeti Boys.
.