Rais Magufuli afafanua sababu ya serikali kusitisha kuajiri watumishi wapya
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli amesema serikali imesitisha zoezi la ajira na upandishwaji vyeo kwa muda mfupi usiozidi miezi miwili kwa ajili ya kuhakiki watumishi wa umma walioajiriwa.
Rais Magufuli alisema hayo jana alipohudhuria sherehe za Jubelee ya miaka 50 ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) pamoja na kuzindua sarafu ya shilingi 50,000 ambayo itakuwa kwenye kumbukumbu ya benki hiyo.
“Serikali ninayoiongoza haina nia ya kuwakatisha tamaa wafanyakazi, lengo lake ni kujipanga kwa makosa tuliyoyafanya, na ndio maana nimesema kwa kipindi cha mwezi mmoja hivi au hata mwezi mmoja na nusu, haitazidi miezi miwili tusiajiri mtumishi yeyote serikalini,” alisema rais Magufuli.
Aidha rais Magufuli aliongeza, “katika kipindi cha mwezi mmoja hatutawapandisha vyeo wafanyakazi, ninaomba wafanyakazi waelewe hili. Kwa sababu tukiendelea tutakuwa tunawapandisha vyeo hata wafanyakazi ambao hawapo, tunafanya ukaguzi wote tukishamaliza wafanyakazi wataendelea kupandishwa vyeo”
Ni takribani miezi mitatu mpaka sasa serikali ikiendelea na zoezi la ukaguzi wa kuwaondoa wafanyakazi hewa huku ikiwa imefanikiwa kuwabaini zaidi ya wafanyakazi hewa 5,000 na kuokoa kiasi cha zaidi ya bilioni 2 zilizokuwa zikilipwa kama mshahara kwa watumishi hewa.