Habari

Waziri Mpango asema hali ya uchumi wa Tanzania inaendelea kukua kwa kasi

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango amesema Tanzania imebaki kuwa miongoni mwa nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara Barani Afrika, ambazo uchumi wake unakua kwa kasi.

Dk Philip Mpango

Dk Mpango alisema hayo jijini Dar es Salaam jana, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hali ya uchumi wa taifa kwa kipindi cha Julai hadi Desemba, 2016 na matarajio hadi Juni, 2017.

Alisema ukuaji wa uchumi ni mojawapo ya vitu vinavyotazamwa katika kutathmini afya ya uchumi wa taifa.

Akifafanua, alitoa mfano kwa baadhi ya nchi hizo kuwa mwaka jana Tanzania uchumi wake ulikuwa kwa asilimia 7.0 na mwaka huu unakua asilimia 7.2, Kenya mwaka jana ulikua asilimia 5.6 na mwaka huu unakua asilimia 6.0, Uganda mwaka jana ulikuwa asilimia 4.8 na mwaka huu unakuwa asilimia 4.9.

“Kwa mifano hiyo tunaona Tanzania imeendelea kufanya vizuri uchumi unakuwa kwa kasi kubwa katika Bara la Afrika,” alisema.

Kwa upande mwingine, alisema kuwa ustawi wa uchumi wa taifa unapimwa kwa kuangalia viashiria mbalimbali vikiwemo ukuaji wa pato la taifa, mfumko wa bei, thamani ya shilingi, mwenendo wa sekta ya kibenki na sekta ya nje na akiba ya fedha za kigeni.

Akizungumzia mfumuko wa bei, alisema ulipungua kutoka asilimia 6.5 Januari 2016 hadi asilimia 5.5 Juni 2016 na kupungua zaidi hadi asilimia 4.5 Septemba mwaka huu. Baadaye ulipanda kidogo mwezi Novemba na kufikia asilimia 4.8.

“Maana yake ni kuwa bei za bidhaa na huduma ziliongezeka kwa kasi ndogo zaidi ikilinganishwa na kipindi cha nyuma. Mwenendo huu wa kushuka kwa mfumuko ulichangiwa na kasi ndogo ya ongezeko la bei za chakula nchini, kushuka kwa bei za mafuta ya petroli katika soko la dunia, utekelezaji madhubuti wa sera za bajeti na fedha na utulivu wa thamani ya shilingi. Kupanda kwa mfumuko wa bei mwezi Novemba kulitokana na kupungua kwa upatikanaji wa bidhaa za chakula pamoja na mkaa,” alisema.

Alisema thamani ya shilingi ya Tanzania imeendelea kuimarika dhidi ya dola ya Marekani. Shilingi imekuwa ikibadilishwa kwa kati ya shilingi 2,167 hadi 2,199 kwa dola moja ya Marekani.

“Hali hii ilitokana na kuwa na sera thabiti za uchumi pamoja na mwenendo mzuri wa urari wa mapato ya fedha za kigeni hususan kutokana na mauzo ya bidhaa za viwandani, utalii na huduma mbalimbali,” alisema.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents