Mike Tyson aja Tanzania
Bingwa wa zamani wa ndondi katika uzito wa juu duniani, Iron Mike Tyson, anatarajiwa kutua nchini Septemba mwaka huu akiambatana na bondia Laila Ali, ambaye ni binti wa nguli wa masumbwi duniani, Muhammed Ali
BINGWA wa zamani wa ndondi katika uzito wa juu duniani, Iron Mike Tyson, anatarajiwa kutua nchini Septemba mwaka huu akiambatana na bondia Laila Ali, ambaye ni binti wa nguli wa masumbwi duniani, Muhammed Ali.
Wakati Tyson akiwa amestaafu ndondi, Laila ni miongoni mwa mabondia mahiri wa kike wanaotamba duniani kwa sasa, hivyo kufuata nyayo za baba yake.
Akizungumza katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), jijini Dar es Salaam jana, mratibu wa ujio huo, Zuwena Kibene, alisema mabondia hao wanakuja kwa mwaliko rasmi wa kutoa semina kwa mabondia wa Tanzania.
Alisema, kutokana na ujio huo, anatarajia kuanza ziara ya kuzunguka nchi nzima ili kuhamasisha mabondia kufika katika mikoa ya jirani ambako wageni hao wataifikia.
Kibene aliitaja mikoa ambayo mabondia hao wataifikia, ni Dar es Salaam, Arusha na Mwanza, hivyo amewataka mabondia wa jirani na mikoa hiyo, kufika katika mikoa hiyo kwa gharama zao.
Alisema, mabondia watakaokuwa wakitoka nje ya mikoa hiyo, watajigharamia usafiri, huku yeye (Kibena), akigharamia malazi, chakula na nauli za kurejea makwao.
Alipoulizwa kama mabondia hao watacheza pambano lolote, alisema hawatacheza pambano lolote kwani hakuna anayeweza kupambana nao.
Alisema, kitakachofanyika ni mabondia hao kutoa mafunzo kabla ya kushuhudia mapambano ya mabondia mbalimbali wa hapa nchini.
Tyson, mbabe aliyetamba vilivyo katika ulimwengu wa masumbwi duniani, ni miongoni mwa mabondia walio na mashabiki wengi kutokana na umahiri na vituko vyake.
Miongoni mwa kituko kinachokumbukwa, ni pale alipomngÂ’ata sikio bondia mwenzake, Evander Hollyfield katika kuwania ubingwa wa dunia.
Source: Tanzania Daima