Msumbiji yakana kuhusika na mlipuko Lebanon
Mamlaka ya bandari nchini Msumbiji imekanusha kufahamu kuhusu meli ya Rhosus iliyobeba tani 2,750 za ammonium nitrate na kusababisha mlipuko Beirut.
Hayo yameelezwa wakiwa wanajibu taarifa zinazoenea kuwa meli hiyo ilikuwa katika bandari hiyo ya Beirut tangu mwaka 2013 ikiwa imetoka safari yake Georgia na kuelekea mji wa kati wa bandari ya Beira, Msumbiji kisha kukwama hapo Lebanon na kushusha mizigo.
Mnamo mwaka 2013 meli inayopeperusha bendera ya Moldova, Rhosus iliingia katika bandari ya Beirut baada ya kuwa na matatizo ya kiufundi wakati ikiwa safarini kutoka Georgia kuelekea nchini Msumbiji, kwa mujibu wa Mamlaka ya bandari inayofuatilia mienendo ya Meli.
“Kiongozi wa bandari hiyo hakuwa na taarifa ya meli ya MV Rhosus itaingia kwenye bandari ya Beira,” mamlaka ya bandari ya Beira ilisema katika taarifa.
Mlipuko huo katika bandari ya Beirut, Lebanon umesababisha vifo vya watu 137 huku 5,000 wakijeruhiwa. Inadaiwa meli hiyo ilibeba tani 2,750 za ammonium nitrate zilizo hifadhiwa katika bandari hiyo tangu 2013 bila kuzingatia usalama.