Mzee Kilomoni avuliwa uanachama wa Simba SC
Klabu ya Simba leo Agosti 13 kupitia mkutano wa kamati ya Utendaji imeamuru kumtoa katika Baraza la Udhamini, Mzee Hamis Kilomoni baada ya kufungua kesi mahakamani ikiwa ni kinyume na katiba ya klabu hiyo.
Akizungumza kwenye mkutano huo Kaimu rais wa klabu hiyo, Salim Abdallah amesema kuwa baada ya Kamati ya Utendaji kukaa na kujadili suala hilo, wamefikia maamuzi ya kumtoa katika Baraza la Wadhamini Mzee Kilomoni baada ya kufungua kesi mbili mfululizo dhidi ya klabu hiyo.
“Kamati imefikia hatua hii baada ya kuona kuwa Mzee wetu anakiuka miiko, hivyo tumeona kuwa tunamtoa na nafasi yake inachukuliwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Adam Mguhi, huyu ni mtu sahihi kwetu”,amesema Abdallah.
Hata hivyo, kamati ya utendaji imemsimamisha uanachama Mzee Kilomoni na itamuandikia barua ya kumsimamisha, huku wakisubiria kujitetea kwake na kufuta kesi mahakamani na asipofanya hivyo atakuwa amejitoa moja kwa moja uanachama
Kwa upande mwingine kamati hiyo imepitisha jina la Juma Kapuya kuwa mmoja wa wadhamini katika Baraza la Wadhamini, akichukua nafasi ya Ally Sykes ambaye amefariki dunia.