Nchi zilizosaini mkataba wa nyuklia na Iran kukutana
Mataifa yaliyosaini mkataba wa nyuklia wa Iran yanakutana hii leo mjini Vienna, katika wakati ambapo Marekani ikishinikiza taifa hilo la Kiislamu lirejeshewe vikwazo na jumuiya ya kimataifa na kuongezewa vizuizi vya silaha.
Uingereza, Ufaransa, Ujerumani, China na Urusi wanajaribu kuunusuru mkataba huo wa mwaka 2015 na Iran, ambayo imekuwa inaongeza shughuli zake za kinyuklia tangu mwaka jana.
Mkutano huo utaongozwa na afisa wa ngazi za juu wa umoja wa Ulaya Helga-Maria Schmid pamoja na manaibu waziri wa mambo ya kigeni ama wakurugenzi wa masuala ya siasa watakaohudhuria kutoka Uingereza, China, Ufaransa, Ujerumani, Iran na Urusi.
Umoja wa Mataifa wiki iliyopita ulizuia jaribio la Marekani la kurejesha vikwazo vya kimataifa dhidi ya Iran huku Washington ikishindwa kupata uungwaji mkono wa kuongeza vikwazo vya silaha kwa taifa hilo.